T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 07 Jul 2026 23:55:33

Mapambano bado, wasema mashujaa wa Saba Saba

MIAKA 36 baada ya maandamano ya kihistoria ya Saba Saba ya Julai 7, 1990, baadhi ya viongozi walioongoza mapambano ya kurejesha mfumo wa vyama vingi vya kisiasa wanasema safari ya kupigania utawala bora bado haijakamilika. Viongozi hao walikumbuka jinsi walivyokabiliana na ukandamizaji wa utawala wa aliyekuwa Rais Daniel arap Moi, huku wakisema hali iliyoshuhudiwa Jumanne ya kufungwa kwa barabara na kumwagwa kwa polisi wengi mijini iliwakumbusha matukio ya miaka hiyo. Katika Saba Saba ya kwanza, serikali ya Moi ilizuia mkutano uliokuwa umeitishwa katika Uwanja wa Kamukunji, Nairobi na viongozi Kenneth Matiba na Charles Rubia. Kabla ya mkutano huo, Matiba, Rubia na Raila Odinga walikamatwa na kuzuiliwa, lakini wanaharakati waliendelea na maandamano licha ya msako mkali wa vitengo vya usalama. Shinikizo lililotokana na maandamano hayo lilichangia kufutwa kwa Kifungu cha 2A cha Katiba mwaka wa 1991 na kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi vya kisiasa. Miongoni mwa waliokuwa mstari wa mbele katika mapambano haya walikuwa Odinga, James Orengo, Paul Muite, Gitobu Imanyara, Kiraitu Murungi, Njeru Kathangu, Mukhisa Kituyi, Martin Shikuku na Masinde Muliro, pamoja na viongozi wa kidini akiwemo Askofu Ndingi Mwana a'Nzeki, Mchungaji Timothy Njoya, Askofu David Gitari, Henry Okullu na Alexander Muge. Gavana wa Siaya, Orengo, ambaye alijiunga na maadhimisho ya Saba Saba jijini Nairobi jana, alisema ni jambo la kusikitisha kuwa taifa hili bado halijatenga siku rasmi ya kuwaenzi mashujaa wa mapambano ya ukombozi wa pili. "Kama ningekuwa rais chini ya Katiba hii mpya, ningetangaza Saba Saba kuwa siku ya kitaifa ya kuwaenzi watu kama Kenneth Matiba, Charles Rubia na Raila Odinga," alisema. Aliyekuwa mbunge wa Runyenjes, Kathangu, alisema kurejeshwa kwa vyama vingi hakukuleta mageuzi yote yaliyotarajiwa kwa sababu wengi wa wanaharakati walikuwa gerezani wakati vyama vipya viliposajiliwa. "Tulitarajia Wakenya wapate viongozi wapya, lakini wengi wetu tulikuwa kizuizini. Vijana wa Gen Z wanapaswa kuendelea kupigania utawala bora kama tulivyofanya mwaka wa 1990," alisema. Kwa upande wake, wakili Muite alisema mapambano ya Saba Saba yalizaa matunda makubwa, ikiwemo Katiba ya mwaka wa 2010 ambayo imeimarisha haki na uhuru wa wananchi. Alisema Wakenya, hasa vijana wa Gen-Z, wameonyesha ujasiri mkubwa wa kuwawajibisha viongozi na kusisitiza kuwa ukiukaji wa haki za binadamu lazima uwajibishwe watu. Hata hivyo, kiongozi wa ODM, Oburu Oginga alisema Saba Saba haipaswi kuwa siku ya maandamano ya barabarani bali ya kutafakari mafanikio yaliyopatikana tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi. Naye Seneta wa Kitui, Enoch Wambua alisema Saba Saba inaendelea kuwa ukumbusho wa mapambano ya demokrasia na utawala bora, akiongeza kuwa vijana wa sasa wamechukua nafasi ya kizazi kilichopigania mageuzi miaka ya 1990 katika kudai uongozi wajibifu.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 07 Jul 2026 22:55:33

Mombasa yaweka mfano bora wa maandamano yaliyojaa amani

HUKU ulinzi mkali ukiwekwa sehemu nyingi nchini kwa hofu ya vurugu wakati wa maadhimisho ya Saba Saba, Mombasa iliendelea kujitokeza kama mfano wa jinsi maandamano yanavyoweza kufanyika kwa amani bila matumizi ya vitoa machozi, kukamatwa kwa waandamanaji au uharibifu wa mali. Kwa mwaka wa pili mfululizo, waandamanaji katika jiji hilo la pwani waliandamana kwa utulivu, wakipinga dhana kwamba maandamano lazima yaambatane na vurugu, maafa na uharibifu wa mali. Tofauti na ilivyoshuhudiwa katika maeneo mengine, hakukuwa na taarifa za watu kupigwa, kukamatwa au polisi kutumia vitoa machozi. Aidha, hakukuwa na vizuizi vya barabarani katika njia kuu zinazoingia na kutoka katikati mwa jiji la Mombasa. Biashara ziliendelea kama kawaida, magari ya uchukuzi wa umma yaliendelea na shughuli zake huku waandamanaji wakipita katika barabara kuu wakipaza sauti za kutetea demokrasia na uhuru. Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Mombasa Nicholas Chalulot, alisema maandamano ya amani hayawezekani bila maandalizi ya kina na mawasiliano ya karibu kati ya waandalizi na maafisa wa usalama. "Maandamano ya amani yanaweza kuvamiwa na wahuni, hivyo huwa tupanga mapema na kuhakikisha polisi wapo kila mahali. Uwepo wao huwazuia wanaotaka kuvuruga maandamano," alisema. Aliongeza kuwa mazungumzo kati ya polisi na waandalizi hufanyika kabla na wakati wa maandamano ili kutatua tofauti zozote zinazojitokeza. "Tunakubaliana, wakati mwingine hatukubaliani, lakini mwisho wa siku tunafikia mwafaka na maandamano huendelea kwa amani," alisema. Alisema pia maafisa wa polisi hupewa maelekezo ya kutowachokoza waandamanaji. "Wasipochokozwa, uwezekano wa vurugu hupungua sana," aliongeza. Kwa upande wake, mratibu wa Mtandao wa Mashirika ya Kijamii ya Pwani kuhusu Haki za Kibinadamu, Aisha Khamis, alisema mafanikio ya maandamano hayo huanza na maandalizi ya muda mrefu. Kulingana naye, ujumbe unaotumwa kupitia WhatsApp na mitandao mingine ya kijamii huwa mmoja: watu wahudhurie na kudumisha amani, wasibebe silaha na wakumbuke kuwa lengo ni kufikisha ujumbe, si kupambana na polisi. "Barabara si uwanja wa vita. Tunakuja kutoa ujumbe na kuwaenzi waliopigania nafasi ya kidemokrasia tunayofurahia leo," alisema. Naye mwanaharakati Lydia Adhiambo alisema waandalizi huwafahamisha polisi mapema kuhusu njia watakazotumia na maeneo ya kukusanyika, jambo ambalo limechangia kudumisha utulivu.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 07 Jul 2026 21:55:20

Hasara tele baada ya serikali kufunga barabara kuu kuzima maandamano ya Saba Saba

ILIKUWA hasara tele baada ya serikali kufunga baadhi ya barabara kuu zinazoingia Nairobi na kuimarisha usalama kuzima maandamano ya Saba Saba jana. Maelfu ya wasafiri walikwama asubuhi baada ya polisi kufunga kwa muda baadhi ya barabara kuu na kuzuia magari mengi ya uchukuzi wa umma kuingia jijini Nairobi. Hatua hiyo ilisababisha foleni ndefu za abiria katika vituo vya mabasi huku wengi wakishindwa kufika kazini, wafanyabiashara wakakosa wateja na shughuli nyingi za kiuchumi kusimama kutokana na ukaguzi mkali uliowekwa katika maeneo mbalimbali kwenye barabara za Thika, Jogoo, Mombasa na Waiyaki Way. Polisi waliweka vizuizi katika maeneo ya Kimbo, Kihunguro na makutano ya Barabara ya Eastern Bypass kwenye Barabara ya Thika, ambako walikuwa wakisimamisha na kukagua magari yaliyokuwa yakielekea Nairobi. Magari ya kibinafsi yaliruhusiwa kuendelea na safari baada ya kukaguliwa, lakini matatu nyingi zilizuiwa kuingia barabara hiyo, hali iliyowaacha mamia ya abiria bila usafiri. Kufungwa kwa baadhi ya sehemu za Barabara ya Thika na Mombasa Road pia kulisababisha msongamano mkubwa wa magari, huku matatu chache zilizohudumu zikikataa kuelekea katikati mwa jiji la Nairobi kwa kuhofia vizuizi vilivyowekwa na polisi. Maduka yalifungwa jijini huku shughuli za masomo zikitatizwa walimu wakiagiza wazazi kukaa na watoto wao nyumbani. Hata usafiri wa wanafunzi kwenda shule haungewezekana kutokana na vizuizi vilivyowekwa na polisi. Biashara nyingi hazikufunguliwa na hata zilizofunguliwa hazikupata wateja. "Nimekuwa hapa kwa saa mbili sasa na hakuna matatu. Zile chache zinazofika zinasema haziendi mjini," alisema Martin Oduor, mmoja wa wasafiri waliokwama katika kituo cha Githurai 45. Alisema hatua hiyo iliwaathiri zaidi watu wanaotegemea mapato ya kila siku ili kujikimu. "Inasikitisha sana. Wengi wetu tunaishi kwa kutegemea kile tunachopata kila siku. Lazima tufike kazini ili tupate riziki, lakini sasa polisi wametuzuia. Siwezi kufika kazini," alisema. Wasafiri wengi walionekana wakisubiri kando ya barabara wakitumaini kupata usafiri mbadala, huku wengine wakiamua kutembea kwa miguu umbali mrefu baada ya kubaini kuwa hawangeweza kupata matatu ya kuelekea jijini. Operesheni hiyo ya usalama ilijiri polisi wakiongeza ulinzi na kudhibiti njia za kuingia Nairobi kabla ya maandamano ya Saba Saba, huku maafisa wa usalama wakimwagwa kwa wingi katika barabara kuu zinazoelekea katika mji mkuu. Hali ilikuwa tulivu katika eneo la Mlolongo kwenye Barabara ya Mombasa licha ya uwepo mkubwa wa maafisa wa polisi waliokuwa kwenye doria kabla ya maandamano hayo. Maafisa wa polisi walikuwa wamepiga kambi katika lango la kuingia na kutoka Barabara ya Expressway eneo la Mlolongo, lakini tofauti na ilivyokuwa Juni 25 wakati wa kumbukumbu ya miaka miwili ya maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha wa 2024, hakukuwa na vizuizi vikubwa barabarani. Siku hiyo ya Juni 25, polisi walikuwa wakikagua kwa makini magari yote yaliyokuwa yakitaka kupita eneo hilo, huku madereva wengi wakielekezwa kurejea walikotoka. Hata hivyo, jana hakukuwa na vizuizi katika sehemu kubwa ya Barabara ya Mombasa isipokuwa katika mzunguko wa Barabara ya Bunyala, ambako maafisa walikuwa wakikagua baadhi ya magari yaliyokuwa yakielekea katikati mwa jiji. Maafisa wengine walionekana wakishika doria katika maeneo mbalimbali, yakiwemo lango la Expressway Mlolongo, makutano ya Mlolongo na Kitengela, mzunguko wa Barabara ya Bunyala pamoja na makutano ya Barabara ya Haile Selassie na Uhuru Highway. Licha ya uwepo huo wa polisi, shughuli za usafiri ziliendelea kwa utulivu huku msongamano wa magari ukiwa mdogo kuliko ilivyo kawaida kwenye Barabara ya Mombasa. Wakati huo huo, kiongozi wa Chama cha People's Liberation Party (PLP), Martha Karua, alikosoa hatua ya serikali ya kufunga baadhi ya barabara nchini. Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ofisi ya chama hicho katika eneo la Nyamataro, Kaunti ya Kisii, Bi Karua alisema Wakenya hawapaswi kuzuiwa kutoa maoni yao au kutumia haki zao za kikatiba mradi wanafanya hivyo kwa amani. "Serikali haipaswi kuweka vizuizi vya barabarani kama ilivyofanya leo katika maeneo mbalimbali nchini. Ni jambo la kusikitisha. Tulinde amani huku tukiheshimu haki na uhuru wa wananchi," alisema. Kaunti ya Embu nayo ilishuhudia taharuki huku polisi wa kutuliza ghasia waliokuwa wamejihami kwa silaha wakishika doria mjini humo kabla ya maandamano ya Saba Saba. Maafisa hao walionekana wakizunguka katika mitaa mbalimbali huku wafanyabiashara wengi wakiendelea na shughuli zao kama kawaida. Hata hivyo, baadhi ya wafanyabiashara hawakufungua maduka yao asubuhi kwa hofu kwamba huenda maandamano yangesababisha vurugu. Katika Barabara Kuu ya Embu-Makutano, polisi waliweka vizuizi na kuwakagua madereva pamoja na magari yaliyokuwa yakitumia njia hiyo ili kuhakikisha hayakusafirisha wahuni waliokusudia kuvuruga amani. Ukaguzi huo ulisababisha msongamano wa magari katika barabara hiyo ambayo kwa kawaida huwa na shughuli nyingi. Aidha, wasafiri waliokuwa wakielekea Nairobi walikwama katika kituo cha mabasi cha Embu baada ya wahudumu wa matatu kususia safari kuelekea mji mkuu kwa kuhofia hali ya usalama. Baadhi ya wasafiri hao walilazimika kukatiza safari zao na kurejea nyumbani baada ya kubaini hawangeweza kupata usafiri wa kuelekea Nairobi.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 07 Jul 2026 22:25:03

Maandamano yatikisa elimu, wanafunzi wakikosa kuenda shule

MAELFU ya wanafunzi nchini wameendelea kupoteza muda muhimu wa masomo kutokana na kufungwa kwa shule kila kunapozuka maandamano ya kisiasa, huku wazazi wengi wakiamua kusalia na watoto nyumbani kwa hofu ya usalama. Shule zilizo katika maeneo ya mijini ndizo zimeathirika zaidi, hasa zile zilizo karibu na maeneo ambayo waandamanaji hukabiliana na polisi. Miongoni mwa shule hizo ni Moi Avenue Comprehensive School katikati mwa jiji la Nairobi, Jamhuri High School na St Brigid's Public Primary School. Shule nyingine katika kaunti za Machakos, Kiambu, Mombasa, Kisumu na Nakuru pia zimeripoti kusitisha masomo kila kunapoandaliwa maandamano kutokana na hofu ya usalama. "Mimi sikuwapeleka watoto wangu shuleni licha ya serikali kusema ni siku ya kawaida ya kazi. Hatari ilikuwa kubwa mno," alisema mzazi wa Nairobi, Nelly Koki. Katika maandamano ya kuadhimisha Saba Saba, shule kadhaa zilisitisha masomo ya darasani. Baadhi ziliwaagiza wazazi kuwa na watoto nyumbani, nyingine zikaendesha masomo mtandaoni huku baadhi zikiwapa kazi za kufanyia nyumbani. Ingawa Wizara ya Elimu haikutoa agizo la kitaifa la kufunga shule, wasimamizi wengi wa shule walisema walichukua hatua hiyo kama tahadhari kutokana na hali ya usalama na changamoto za usafiri. Huduma ya Kitaifa ya Polisi ilitangaza kuwa kutakuwa na ukaguzi mkali wa watu na magari katika barabara mbalimbali za Nairobi ili kuhakikisha amani inadumishwa. Taarifa a zilionyesha shule ziliwafahamisha wazazi kuwa masomo yangeendelea kupitia kazi za nyumbani ili kuwatayarisha wanafunzi kwa mitihani ya mwisho wa muhula. Hii si mara ya kwanza. Wakati wa maandamano ya upinzani wa 2023 na yale ya kupinga Mswada wa Fedha wa 2024, shule nyingi zilifungwa kwa muda huku baadhi zikiahirisha kufunguliwa baada ya likizo ya katikati ya muhula. Maandamano hayo pia yaligharimu maisha ya wanafunzi wa vyuo vikuu na shule, hali iliyoibua wasiwasi kuhusu usalama wa wanafunzi wakati wa misukosuko ya kisiasa.

read more