T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 12 Jul 2026 03:55:21

Mwanajeshi apatikana na hatia ya kuua mkewe na wanawe kambini

BAADA ya takriban miaka saba ya kusubiri haki, Mahakama Kuu jijini Nairobi Ijumaa ilihitimisha moja ya kesi zilizotikisa taifa kwa kumpata aliyekuwa Meja wa Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF), Peter Mugure Mwaura, na hatia ya kumuua mkewe Joyce Syombua pamoja na watoto wao wawili. Jaji Martin Muya alisema upande wa mashtaka ulithibitisha bila shaka yoyote kwamba Mugure alipanga mauaji hayo kwa umakini, akayatekeleza ndani ya Kambi ya Jeshi la Anga ya Nanyuki, kisha akashirikiana na mtu mwingine kuficha miili ya marehemu kwa kuizika eneo la Thigithu, Kaunti ya Laikipia. Kulingana na ushahidi uliowasilishwa mahakamani, Joyce, mwenye umri wa miaka 31, alisafiri kutoka Nairobi hadi Nanyuki Oktoba 25, 2019 akiwa na watoto wake Shanice Maua, 10, na Prince Michael, 5, baada ya Mugure kuwaalika kwa kile kilichoonekana kuwa mkutano wa kifamilia. Siku iliyofuata walionekana wakiondoka kambini pamoja kabla ya kula chakula cha mchana katika Hoteli ya Kilimara Springs. Huo ndio ulikuwa mwisho wao kuonekana wakiwa hai. Jaji Muya alisema baada ya kurejea kambini, Mugure aliwaua watatu hao, akaweka miili yao kwenye mifuko maalumu ya kuhifadhia maiti na kuificha kwenye buti la gari lake kabla ya kwenda kuizika kwa siri Thigithu. Mahakama ilisema mauaji hayo hayakuwa ya ghafla. Ushahidi ulionyesha kuwa siku tatu kabla ya tukio, Mugure alikuwa ametembelea eneo hilo akiwa na afisa mwingine, hatua ambayo ilimshawishi jaji kuwa tayari alikuwa amechagua mahali pa kuficha miili kabla ya kutekeleza mpango wake. Shahidi muhimu katika kesi hiyo alikuwa Collins Pamba, aliyekiri kusaidia kuondoa miili. Alieleza kuwa alipofika nyumbani kwa Mugure alikuta mwili wa Joyce ukiwa ndani ya mfuko wa maiti huku miili ya watoto ikiwa kwenye bafu. Alisema walifunga miili kwa kamba, wakaiweka ndani ya buti la gari baada ya kuondoa tairi la akiba ili kupata nafasi zaidi, kisha wakaitoa kambini na kuizika. Ingawa alikiri kushiriki kuficha ushahidi, Pamba alifanya makubaliano na upande wa mashtaka, akakiri kosa dogo na kuhukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani. Jaji alisema ushahidi wake uliungwa mkono na ushahidi wa kisayansi. Uchunguzi wa DNA uliofanywa na Mkemia Mkuu wa Serikali ulithibitisha kuwa mabaki yaliyopatikana kaburini yalikuwa ya Joyce, Shanice na Prince Michael. Aidha, vipimo vilionyesha kwa uwezekano wa asilimia 99.9 kwamba Mugure alikuwa baba wa watoto hao wawili. Ripoti ya uchunguzi wa maiti ilionyesha Joyce alifariki kutokana na majeraha makubwa ya kupigwa, huku watoto wote wawili wakinyongwa. Mahakama pia ilibaini kuwa kulikuwa na sababu ya kifedha nyuma ya mauaji hayo. Joyce alikuwa amepata amri ya mahakama iliyomtaka Mugure kulipa Sh25,000 kila mwezi kama matunzo ya watoto, lakini alilipa mara moja pekee kabla ya kumshawishi asafiri hadi Nanyuki. Jaji Muya alitupilia mbali utetezi wa Mugure kwamba aliwaacha watoto kwa rafiki wa Joyce, akisema hakuna ushahidi uliounga mkono na kwamba familia hiyo haikuwahi kutoka kambini ikiwa hai. Kwa msingi huo, mahakama ilimpata Mugure na hatia katika mashtaka yote matatu ya mauaji, ikisema upande wa mashtaka ulithibitisha kesi yake bila shaka yoyote. Atahukumiwa Julai 14, 2026.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 12 Jul 2026 02:55:17

Kinaya serikali ikigeuka adui wa kutunza misitu

SERIKALI inaendelea kusukuma mpango wake wa kupanda miti bilioni 15 ifikapo 2032 kama sehemu ya juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kurejesha mazingira yaliyoharibiwa. Hata hivyo, wanaharakati wa mazingira wanaonya kuwa mafanikio ya mpango huo yanaweza kutatizwa na ongezeko la miradi ya maendeleo inayopendekezwa ndani ya misitu asili. Kwa mujibu wa wanamazingira, hali ya sasa inaibua kinaya. Wanasema huku serikali ikihamasisha wananchi kupanda mabilioni ya miche ya miti, sehemu nyingine za misitu inaendelea kukatwa ili kupisha ujenzi wa barabara, reli, viwanja vya ndege, nyumba za serikali na miradi mingine ya miundombinu. Rais William Ruto, ambaye kabla ya kuingia katika siasa alisomea Botania, Zoolojia na Ikolojia ya Mimea katika Chuo Kikuu cha Nairobi, amefanya uhifadhi wa mazingira kuwa mojawapo ya nguzo kuu za utawala wake. Serikali yake imeweka lengo la kupanda miti bilioni 15 ndani ya miaka kumi ili kuongeza kiwango cha misitu nchini na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Hata hivyo, tangu alipoingia madarakani mwaka 2022, serikali imelaumiwa kwa kuruhusu miradi mbalimbali inayopangwa ndani ya misitu. Hali hiyo imezua maswali kuhusu iwapo juhudi za kurejesha mazingira zinaenda sambamba na kulinda misitu ya asili ambayo imekuwepo kwa miongo mingi. Takwimu za ripoti ya hali ya uchumi zinaonyesha kuwa eneo la mashamba ya miti ya serikali liliongezeka kutoka hekari 143,900 mwaka 2021 hadi hekari 148,600 mwaka 2025. Pia kasi ya upanzi wa miti iliongezeka baada ya kuzinduliwa kwa mpango wa kitaifa, huku maelfu ya hekari zikipandwa miche mipya kila mwaka. Lakini wakati huo huo, ukataji wa miti katika mashamba ya serikali ulirejelewa baada ya kuondolewa kwa marufuku ya miaka sita, ingawa baadaye mahakama ilisimamisha uamuzi huo. Kwa wanaharakati wa mazingira, changamoto kubwa si uvunaji wa miti pekee bali kutumiwa kwa misitu asili kwa miradi ya maendeleo. Wanasema kila barabara, njia ya umeme au jengo linalojengwa ndani ya msitu hupunguza uwezo wa mfumo wa ikolojia kuendelea kufanya kazi ipasavyo. Wasiwasi huo uliongezeka baada ya Bunge kupitisha Sheria ya Marekebisho ya Uhifadhi na Usimamizi wa Misitu ya mwaka 2025, ambayo inaruhusu Huduma ya Misitu Kenya (KFS) kutoa nafasi kwa ujenzi wa barabara, njia za umeme na miundombinu mingine ndani ya misitu ya umma. Mojawapo ya miradi iliyozua mjadala mkubwa ni barabara ya Ihithe-Ndunyu Njeru inayopangwa kupita ndani ya Msitu wa Aberdare. Ripoti za tathmini ya mazingira zinaonyesha kuwa ujenzi huo utahitaji kukatwa kwa sehemu ya msitu wa mianzi, msitu wa milimani na maeneo ya nyasi. Wanaharakati wanaonya kuwa Aberdare ni mojawapo ya vyanzo muhimu vya maji nchini, ikihudumia mabwawa ya Sasumua na Ndakaini pamoja na kuchangia uzalishaji mkubwa wa umeme wa maji. Kwa sababu hiyo, Mahakama ya Mazingira ilisimamisha mradi huo kwa muda huku kesi ikiendelea kusikilizwa. Katika Jiji la Nairobi, hofu kama hiyo imejitokeza kuhusu Msitu wa Ngong Road, ambapo sehemu ya ardhi imetengwa kwa miradi inayohusiana na Uwanja wa Talanta. Wanaharakati wanasema ujenzi wa barabara ya kuingia, eneo la wakandarasi na miundombinu mingine unaweza kuendelea kugawa msitu huo katika vipande vidogo. Kadhalika, katika Msitu wa Karura, ukataji wa baadhi ya miti mapema mwaka huu uliibua maswali kutoka kwa wanaharakati. Serikali ilieleza kuwa eneo hilo linatayarishwa kwa vitalu vya miche ya miti na makazi ya muda ya vijana wa Huduma ya Kitaifa kwa Vijana (NYS) wanaoshiriki katika mpango wa kupanda miti. Katibu wa Maendeleo ya Misitu, George Tarus, amesisitiza kuwa serikali haina mpango wa kuharibu misitu asili. Alisema tayari miti takriban1.9 bilioni imepandwa chini ya mpango wa kitaifa na kwamba miradi yote inayopendekezwa ndani ya misitu lazima ifanyiwe tathmini ya athari kwa mazingira kabla ya kuidhinishwa. Kwa mujibu wake, lengo ni kurejesha mazingira yaliyoharibiwa katika misitu, maeneo ya malisho, mashamba na sehemu za kijani mijini, huku maendeleo muhimu yakiendelea kwa kuzingatia sheria za mazingira. Hata hivyo, wanaharakati wanasisitiza kuwa mafanikio ya mpango wa kupanda miti hayatapimwa kwa idadi ya miche iliyopandwa pekee. Wanasema kipimo kikubwa kitakuwa uwezo wa Kenya kulinda misitu yake ya kale na mifumo yake ya ikolojia dhidi ya uharibifu unaoweza kusababishwa na miradi ya maendeleo, ili juhudi za kurejesha mazingira zisiwe zinafutwa na uharibifu unaoendelea katika misitu asili.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 12 Jul 2026 01:55:59

Manifesto za Raila Odinga kuanza kufunzwa chuoni

BAADHI ya manifesto ambazo aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Amolo Odinga alitumia katika kampeni zake za urais zitakuwa sehemu ya masomo katika Chuo cha Uongozi na Utawala cha Raila Amolo Odinga kinachoanzishwa chini ya Chuo cha Serikali Kenya (KSG). Chuo hicho, kilichozinduliwa Jumanne na Rais William Ruto wakati wa maadhimisho ya miaka 100 ya KSG, kinalenga kuhifadhi na kufundisha falsafa za Raila kuhusu utawala bora, demokrasia, huduma kwa umma na maendeleo ya bara Afrika. Mkurugenzi Mkuu wa KSG, Profesa Nura Mohamed, alisema kundi la kwanza la wanafunzi linatarajiwa kuanza masomo mwezi Septemba. Alisema mtaala wa chuo hicho utajengwa juu ya nguzo tano kuu zilizotawala maisha ya kisiasa ya Raila; umoja wa Afrika, uongozi ushirikishi, utawala bora, elimu na ubunifu, pamoja na amani na haki.  "Alipokuwa akiwania urais alikuwa na manifesto mbalimbali, na baadhi yake zitajumuishwa katika masomo ya chuo hiki ili maono yake yaweze kutekelezwa," alisema. Profesa Mohamed alisema walipolinganisha manifesto ya mwisho ya Raila na Ajenda ya Mabadiliko ya Kiuchumi ya Kenya Kwanza, waligundua kuwa zilikuwa na mambo mengi yanayofanana. Kwa mujibu wake, masomo katika chuo hicho yatakitwa kwa kuzingatia maono ambayo Raila alikuwa nayo kwa Kenya na bara la Afrika. Mbali na masomo, chuo hicho kitakuwa na maktaba itakayopewa jina la Raila Odinga pamoja na kituo cha kuhifadhi nyaraka, hotuba, maandishi na mchango wake katika uongozi na siasa. Aidha, kutakuwa na Kituo cha Ubunifu cha Chandaria kitakachofadhiliwa na mfanyabiashara Manu Chandaria, pamoja na Kituo cha Umahiri katika Huduma kwa Wateja na Uzalishaji kitakacholenga kuboresha utendaji wa watumishi wa umma. Profesa Mohamed alisema chuo hicho kinatarajia kuwaalika viongozi mashuhuri duniani kutoa mihadhara ya uongozi, akiwemo Rais wa zamani wa Amerika Barack Obama na marais wa sasa na wa zamani kutoka mataifa mbalimbali. Alisema lengo ni kufanya Kenya kuwa kitovu cha mijadala kuhusu mustakabali wa utawala bora, huduma kwa umma na maendeleo ya Afrika. Kwa mujibu wa kijitabu kinachoelezea malengo ya chuo hicho, taasisi hiyo itakuwa kitovu cha utafiti, ushauri wa sera na ubunifu wa suluhu kwa changamoto kama ufisadi, ukosefu wa ajira, umaskini, maendeleo ya miundombinu na ugatuzi. Pia itaanzisha vituo vya uchambuzi wa sera kwa wizara, Bunge, serikali za kaunti na Mahakama, kuchapisha ripoti za utabiri wa sera na kuandaa taarifa za kila robo mwaka kuhusu uzalishaji katika utumishi wa umma. Profesa Mohamed alisema chuo hicho kitawahudumia mawaziri, makatibu, viongozi waandamizi wa serikali na viongozi wachanga wanaojiandaa kuingia katika sekta ya umma na binafsi. Aliongeza kuwa madarasa ya viongozi wa ngazi za juu yatakuwa na washiriki kati ya 15 na 20 pekee ili kutoa nafasi ya mijadala ya kina kuhusu mikakati ya kubadilisha nchi za Afrika kupitia uongozi bora. Alisema pia chuo hicho kitatoa mpango wa malezi kwa viongozi vijana, ubunifu, afya ya akili kwa watumishi wa umma na kujenga hazina ya kidijitali ya maarifa kuhusu maisha na urithi wa Raila Odinga. "Urithi wa Raila utaendelea kuishi. Tumejizatiti kuhakikisha maono, ndoto na falsafa zake vinaendelea kuongoza juhudi za kuijenga Kenya na kuhamasisha Afrika," alisema Profesa Mohamed.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 12 Jul 2026 00:55:19

Uvumi wa 'kupoteza uume' wazua hofu, vifo na mashambulizi Pwani

KILICHOANZA kama uvumi wa ajabu sasa kimegeuka kuwa chanzo cha hofu, vurugu na vifo katika baadhi ya maeneo ya Pwani, huku polisi na wataalamu wa afya wakikanusha madai kwamba mwanaume anaweza kupoteza sehemu zake za siri baada ya kuguswa na mtu mwingine. Uvumi huo, ambao hauna msingi wa kisayansi wala kitabibu, umefanya watu wengi kuishi kwa wasiwasi. Katika visa kadhaa, watu wasio na hatia wamepigwa na umati wenye hasira baada ya kutuhumiwa kwa madai hayo, huku wahalifu wakidaiwa kutumia taharuki hiyo kuiba simu, pochi na mali nyingine. Kisa kilichotikisa wengi kilitokea Nyali, Mombasa, ambapo waumini wa dhehebu ya Jehovah Witness wanne walishambuliwa walipokuwa wakihubiri kutoka nyumba moja hadi nyingine. Umati uliwalaumu kwa kuhusika na "kupotea" kwa sehemu za siri za wanaume kabla ya polisi kuwaokoa. Baadaye, wakazi wawili, Al Amin Mgunya Johnson na Kennedy Mersyden Milimo, walifikishwa mahakamani wakikabiliwa na mashtaka ya kuchochea vurugu. Milimo pia alishtakiwa kwa kosa la kumshambulia mmoja wa wahubiri hao. Wote walikana mashtaka na kuachiliwa kwa dhamana. Mzee wa Mashahidi wa Yehova katika Jumba la Ufalme la Bamburi, Martin Henya, alisema madai hayo ni ya uongo na kusisitiza kuwa dhehebu hilo halihusiki kwa njia yoyote na uchawi au nguvu za kishirikina. Huku kesi hiyo ikiendelea mahakamani, familia moja Mombasa inaendelea kuomboleza baada ya John Kaleghe, mwenye umri wa miaka 24, kuuawa kwa kupigwa na umati katika Soko la Marikiti baada ya kutuhumiwa kwa madai hayo. Msemaji wa familia, Leah Mwandaghina, alisema Kaleghe alikuwa kitindamimba na tumaini la wazazi wake. Alisema familia ilimtafuta kwa siku kadhaa kabla ya kupata mwili wake katika chumba cha kuhifadhi maiti cha Hospitali ya Rufaa ya Pwani. Kwa mujibu wake, majeraha aliyopata yalikuwa makubwa kiasi kwamba ilikuwa vigumu kumtambua. Familia pia inadai kuwa alikimbilia polisi kuomba msaada lakini hakufaulu kuokolewa kwa umati. Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) Pwani imesema tayari imerekodi visa 19 vinavyohusiana na uvumi huo katika kaunti za Mombasa, Kilifi na Kwale. Watu wawili tayari wameuawa kwa kupigwa na umma. Mratibu wa DCI Pwani, Benson Kasyoki, alisema watu wote waliodai kupoteza sehemu zao za siri walifanyiwa uchunguzi wa kitabibu na kubainika hawakuwa na jeraha lolote wala mabadiliko ya viungo vyao. Alisema uchunguzi unaonyesha makundi ya wahalifu yanatumia uvumi huo kuwalenga watu, huku washirika wao wakiiba mali wakati umati unamzingira mtuhumiwa. Wakati huo huo, DCI imeanzisha uchunguzi wa video za CCTV na ujumbe unaosambazwa mitandaoni ili kubaini wanaochochea vurugu na kusambaza taarifa za uongo. Daktari wa mfumo wa mkojo, Dkt Omar Bin Salman wa Kliniki ya Mombasa Urology, alisema kisayansi haiwezekani kwa sehemu za siri za mwanaume kutoweka kwa kuguswa na mtu mwingine. Alifafanua kuwa mabadiliko ya muda yanayoweza kutokea hutokana na misuli ya mwili kujikaza, lakini haimaanishi kuwa kiungo kimepotea. Aliongeza kuwa kama sehemu hizo zingetoweka kweli, mgonjwa hangeweza kuenda haja ndogo na hiyo ingekuwa hali ya dharura inayohitaji matibabu ya haraka. Kwa sasa, maafisa wa usalama wanatoa wito kwa wananchi kupuuza uvumi huo, kutochukua sheria mikononi na kuripoti visa vyovyote kwa polisi.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 11 Jul 2026 21:55:27

Siasa za ubabe: Pesa itaongea katika uchaguzi wa 2027

IKIWA kuna jambo ambalo wachambuzi wa siasa wanakubaliana nalo, ni kwamba uchaguzi mkuu wa 2027 unatarajiwa kuwa wa gharama kubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa nchini. Kuanzia matumizi ya helikopta za kukodi, wataalamu wa kampeni, mikakati ya kidijitali hadi kampuni za tafiti za maoni, siasa zimegeuka kuwa biashara inayohitaji mabilioni ya fedha. Hali hii imezua hofu kwamba demokrasia inageuka kuwa uwanja wa matajiri na wafadhili wao pekee. Kutokana na hali hiyo, Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imependekeza kanuni mpya za kudhibiti matumizi ya fedha za kampeni ili kuongeza uwajibikaji na uwazi. Chini ya mapendekezo hayo yaliyochapishwa Julai 6, 2026, mgombea urais ataruhusiwa kutumia hadi Sh4.44 bilioni katika kampeni, huku vyama vya kisiasa vinavyowasilisha wagombea kuanzia udiwani hadi urais vikipewa matumizi ya juu ya Sh17.7 bilioni. Wagombeaji wa ugavana, useneta na uwakilishi wa wanawake watatumia kati ya Sh12.3 milioni na Sh123 milioni kulingana na ukubwa wa eneo lao, huku wagombeaji wa ubunge wakiruhusiwa kutumia kati ya Sh17.5 milioni na Sh123 milioni. Wagombea udiwani watatakiwa kutumia kiwango cha juu cha kati ya Sh2.5 milioni na Sh20 milioni. Mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon alisema kanuni hizo zinalenga kuhakikisha fedha za kampeni zinatumika kwa uwazi na uwajibikaji. Hata hivyo, kabla ya kanuni hizo kuanza kutekelezwa, mjadala kuhusu matumizi ya fedha umechacha, hasa kufuatia kampeni za uchaguzi mdogo wa Ol Kalou. Viongozi wa upinzani wakiongozwa na Rigathi Gachagua wameshutumu serikali kwa kutumia fedha nyingi na rasilimali za umma kushawishi wapigakura. "Maafisa wa serikali Ol Kalou ni wengi kuliko wapigakura. Helikopta zimejaa angani kiasi cha karibu kugongana," alisema Bw Gachagua. Katika taarifa ya pamoja, David Maraga, Kalonzo Musyoka, Martha Karua, Fred Matiang'i na Edwin Sifuna walidai vitendo hivyo vinakiuka Sheria ya Makosa ya Uchaguzi, ikiwemo kutoa hongo kwa wapigakura na matumizi ya rasilimali za umma kisiasa. Lakini msemaji wa serikali Isaac Mwaura alitaja madai hayo kuwa ya kupotosha, huku Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung'wah akidai ni ya uongo na propaganda. Mbali na kampeni zinazoonekana hadharani, kuna mtandao mkubwa wa wafadhili ambao hufadhili wagombeaji kwa siri licha ya sheria kuwataka kujitokeza wazi. Katika uchaguzi wa 2022, aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta aliwashawishi wafanyabiashara wa eneo la Mlima Kenya chini ya Mt Kenya Foundation kumuunga mkono Raila Odinga kupitia michango ya mabilioni ya fedha. Kwa upande mwingine, viongozi wa muungano wa upinzani wanakiri kuwa kukabiliana na nguvu za kifedha za serikali iliyoko madarakani ni changamoto kubwa. Profesa Karuti Kanyinga wa Chuo Kikuu cha Nairobi amewahi kukadiria kuwa kampeni za urais nchini hugharimu takriban Sh14 bilioni. Hata hivyo, Martha Karua anasema uchaguzi haupaswi kuamuliwa na fedha bali uadilifu na uwezo wa mgombeaji. Si mashindano ya fedha. Wakenya wanapaswa kuwachagua viongozi kwa tabia, rekodi na uwezo wao wa kuhudumia wananchi," alisema. Aliongeza kuwa chama chake hakitakopa wala kutumia rasilimali za umma kufadhili kampeni. Nao Dkt Fred Matiang'i, Seneta Okong'o Omogeni na aliyekuwa Waziri Mithika Linturi wameeleza wasiwasi kuhusu matumizi makubwa ya fedha na helikopta katika chaguzi ndogo za hivi majuzi. Mashirika ya kutetea demokrasia yameonya kuwa sheria za kufadhili kampeni tayari zipo lakini hazitekelezwi ipasavyo. Mkurugenzi wa Centre for Multiparty Democracy (CMD), Frankline Mukwanja, amesema IEBC inapaswa kusimamia kikamilifu utoaji wa taarifa za michango na matumizi ya kampeni kwa wakati halisi pamoja na kuwaadhibu wanaokiuka sheria. Kwa upande wake, mratibu wa Elections Observation Group (ELOG), Mulle Musau, alisema Sheria ya Ufadhili wa Kampeni ya mwaka 2013 tayari inaeleza vyanzo vinavyoruhusiwa vya fedha na inawataka wagombeaji kufichua wafadhili wao. Mchambuzi wa siasa Mark Bichachi anaamini upinzani utahitaji kutumia teknolojia zaidi kuliko fedha ili kushindana na serikali, huku Profesa Gitile Naituli akisisitiza kuwa ingawa fedha ni muhimu, hazitoshi kushinda uchaguzi. Bila utekelezaji madhubuti wa sheria na uwazi kuhusu fedha za kampeni, wadau wanaonya kuwa uchaguzi wa 2027 unaweza kutawaliwa na nguvu ya fedha badala ya sera, uongozi na maslahi ya wananchi.

read more