T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Wed, 08 Jul 2026 08:58:01

Jinsi ya kulima maparachichi ya masoko ya ng'ambo  

KILIMO cha maparachichi kimekuwa miongoni mwa biashara zenye faida kubwa nchini Kenya kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya matunda hayo katika masoko ya ndani na nje ya nchi. Masoko ya kimataifa, yaani ng'ambo, yamekuwa yenye mvuto mkubwa kwa maparachichi, maarufu kama avokado. Bara Uropa, nchi za Milki ya Kiarabu (UAE) na Asia ndio wanunuzi wakuu wa avokado za Kenya. Ili kupata mavuno bora, mkulima anapaswa kuanza kwa kuchagua miche bora iliyothibitishwa kutoka kwa vitalu vinavyoaminika, anashauri Daniel Mwenda, mtaalamu. "Aina maarufu zinazopendekezwa ni Hass na Fuerte kutokana na ubora wa matunda na soko lake," Mwenda anasema. Maparachichi hustawi katika maeneo yenye mvua ya wastani hadi nyingi, udongo wenye rutuba na usiotuamisha maji. Kabla ya kupanda, Mwenda anasema hatua ya kwanza ni kuandaa shimo lenye ukubwa wa karibu sentimita 60 kwa 60 na kuchanganya udongo wa juu na samadi 'iliyooza' vizuri. "Miche ipandwe kwa nafasi ya mita saba hadi nane kati ya mti na mti ili kutoa nafasi ya ukuaji," anashauri mtaalamu huyo. [caption id="attachment_189894" align="aligncenter" width="300"] Maparachichi ya John Mburu, mkulima kutoka Gatundu Kusini, Kaunti ya Kiambu yakipimwa uzani. Picha|Sammy Waweru[/caption] Miaka ya mwanzo, ni muhimu kumwagilia miche maji hasa wakati wa kiangazi, kuweka nyasi za matandazo (mulching) ili kuhifadhi unyevuunyevu na kupunguza magugu, pamoja na kuondoa matawi yaliyokauka au kuathirika na magonjwa. John Mburu ni mkulima wa avokado Gatundu Kusini, Kaunti ya Kiambu na anasema amekumbatia matumizi ya mbolea asili na fatalaiza. "Mahitaji ya mbolea kwenye udongo, mkulima anapaswa kushirikisha mtaalamu ili upimwe kwenye maabara kujua virutubisho vinavyohitajika," mkulima huyo anasema. Wakulima wanapaswa pia kufuatilia wadudu na magonjwa, na kukabiliana na athari hizo kwa mujibu wa vigezo na dawa zilizoidhinishwa kwa minajili ya mazao yanayouzwa nje ya nchi. "Matumizi ya mbinu bora za usimamizi wa mazao, ikiwemo usafi wa shamba na ushauri wa maafisa wa nyanjani, husaidia kupunguza hasara," mtaalamu Mwenda anahimiza. [caption id="attachment_189895" align="aligncenter" width="300"] Mfanyakazi katika kampuni ya Soko Fresh, Thika akikagua avokado zinazooshwa ili kuuzwa nje ya Kenya. Picha|Sammy Waweru[/caption] Mparachichi huanza kuzaa baada ya miaka miwili hadi mine – hilo likitegemea aina ya mche na usimamizi wa shamba. Matunda yanapaswa kuvunwa kwa uangalifu kwa kutumia vifaa vinavyofaa ili kuepuka majeraha yanayoweza kupunguza ubora wake. Kwa wakulima wanaolenga soko la nje, ni muhimu kufuata viwango vya ubora kama GlobalG.A.P., kuhakikisha matunda yanachambuliwa vizuri na kuhifadhiwa katika mazingira yanayodumisha ubora wake.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Wed, 08 Jul 2026 08:18:11

Wakulima wahimizwa kukumbatia nafaka zinazostahimili ukame

MABADILIKO ya tabianchi yameendelea kuathiri uzalishaji wa chakula nchini Kenya kutokana na mvua isiyotabirika, ukame wa mara kwa mara na ongezeko la joto. Hali hii imepunguza mavuno ya mazao ya kawaida kama vile mahindi, hivyo wataalamu wanashauri wakulima kuanza kulima nafaka na mbegu zinazostahimili ukame ili kujenga mfumo wa kilimo unaoweza kuhimili mabadiliko ya hali ya hewa. "Kuna nafaka ndogo ambazo zinahimili athari za tabianchi kama vile ukame na joto, na baadhi yanaweza kuwa kutumika badala ya mahindi," anasema Dkt Ndungu Kabare, mtaalamu wa kilimo na mkulima kutoka Ruiru. Kulingana na Dkt Kabare, mazao kama vile mtama, wimbi, teff, amaranth na chia yanahitaji maji kidogo, hukomaa haraka na yana misimu miwili ya mavuno kwa mwaka. [caption id="attachment_189887" align="aligncenter" width="300"] Mbegu za chia zilizovunwa. Picha|Sammy Waweru[/caption] "Tofauti na mahindi, mazao haya yana uwezo mkubwa kustahimili vipindi virefu vya ukame bila kupungua sana kiuzalishaji," anaelezea mtaalamu huyo. Mbali na kustahimili mabadiliko ya tabianchi, nafaka hizi zina thamani kubwa ya lishe. Zina madini faafu kwa binadamu, vitamini, na antioxidants kwa kiwango cha juu zaidi kuliko baadhi ya nafakaa. Hali kadhalika, nafaka hizo zina kiwango cha chini cha sukari kinachoingia haraka mwilini (glycemic index), hivyo zinafaa kwa watu wenye maradhi ya kisukari na unene kupita kiasi. "Kwa upande wa biashara, soko la mazao haya linaendelea kukua kutokana na ongezeko la watumiaji wanaotafuta vyakula bora kiafya," Dkt Kabare anasema. [caption id="attachment_189888" align="aligncenter" width="300"] Mtama mweupe ambao pia hutumika kupika ugali. Picha|Sammy Waweru[/caption] Viwanda vya kusaga nafaka, watengenezaji wa vyakula vyenye mseto wa virutubisho, mikate na chakula cha mifugo, pia, vinahitaji malighafi hii, huku teff ikipata ikivutia masoko ya kimataifa. Kulingana na Dkt Kabare, kupanua kilimo cha nafaka na mbegu zinazostahimili ukame kutasaidia Kenya kupunguza utegemezi wa mahindi, kuimarisha usalama wa chakula na kuongeza kipato cha wakulima. Aidha, anasisitiza kuwa mafunzo, mbegu bora na uhamasishaji wa wakulima ni muhimu ili mazao haya yakubalike na kulimwa kwa kiwango cha juu nchini.

read more