T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 21 Jul 2026 02:55:28

DPP: Upo ushahidi kifo cha Ojwang kilipangwa mikononi mwa polisi

MKURUGENZI wa Mashtaka ya Umma (DPP) Renson Ingonga ameambia Mahakama Kuu kuwa upande wa mashtaka utawasilisha ushahidi kuonyesha kuwa kifo cha mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang kilipangwa. Bw Ingonga anasema mauaji hayo yalipangwa Bw Ojwang akiwa mikononi mwa polisi, wala si ajali kama ilivyodaiwa awali. Akitoa hoja wakati wa kuanza kwa kesi katika Mahakama Kuu ya Kibera jana, mwendesha mashtaka mkuu msaidizi Gikui Gichuhi alisema ushahidi utaonyesha jinsi maafisa wa polisi walipanga kipigo kilichosababisha kifo cha Ojwang kisha wakajaribu kuficha ukweli. Aliyekuwa Kamanda wa Kituo cha Polisi cha Central, Samson Tallam, anakabiliwa na mashtaka ya mauaji pamoja na maafisa wa polisi James Mukhwana na Peter Kimani. Wengine walioshtakiwa ni raia watatu, John Ngige Gitau, Jim Ambao na Brian Njue, waliokuwa wakizuiliwa katika seli moja na Bw Ojwang. Bw Gichuhi alisema ushahidi wa kimatibabu utaonyesha kuwa Ojwang alipata majeraha mengi mwilini yaliyosababishwa na kupigwa, kinyume na madai ya awali ya polisi kwamba alijijeruhi kwa kujigonga ukutani. Upande wa mashtaka pia ulisema utawasilisha ushahidi unaodaiwa kuonyesha kulikuwa na juhudi za kuharibu uchunguzi, ikiwemo kufutwa kwa picha za kamera za usalama (CCTV) katika kituo cha polisi. Bw Ojwang alikamatwa nyumbani kwake Kakoth, Kaunti ya Homa Bay, Juni 7, 2025 na maafisa wa DCI kufuatia malalamishi kuhusu chapisho la mitandaoni lililomlenga na Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Langat. Baadaye alihamishwa hadi Kituo cha Polisi cha Central, Nairobi, ambako alifariki akiwa rumande. Ripoti ya uchunguzi wa maiti ilibaini alikuwa na majeraha mabaya kichwani, shingoni na sehemu nyingine za mwili, huku wataalamu wakihitimisha kuwa yalitokana na kushambuliwa na si kujidhuru. DPP anasisitiza kuwa washtakiwa wote sita walihusika katika mauaji hayo, huku uchunguzi ukiendelea chini ya Mamlaka Huru ya Kutathmini Utendakazi wa Polisi (IPOA).

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 21 Jul 2026 00:55:36

Miradi ya unyunyizaji maji yalemewa Pwani licha ya uwekezaji wa mabilioni ya pesa

ENEO la Pwani limezidi kubaki nyuma katika uzalishaji wa chakula, licha ya uwekezaji wa mabilioni ya pesa katika mifumo ya kilimo cha unyunyizaji maji shambani katika kaunti mbalimbali za ukanda huo. Katika Kaunti ya Taita Taveta, mifumo ya unyunyizaji ambayo hapo awali iliifanya Taveta kuwa miongoni mwa maeneo muhimu ya uzalishaji wa chakula kufaa Mombasa, Nairobi na Tanzania imeathiriwa na mifereji iliyozibwa na tope, magugu na uchafu, pamoja na kupungua kwa maji katika mito. Serikali ya Kaunti ya Taita-Taveta imekiri kuwa changamoto za usimamizi, mabadiliko ya tabianchi, uwekezaji duni na miundombinu chakavu imepunguza uzalishaji katika kilimo. Hata hivyo, kaunti inapanga kufufua mifumo ya unyunyizaji na kuwahamasisha vijana kuchukulia kilimo kama taaluma yenye faida. "Ukosefu wa rasilimali za kutosha umeathiri ukarabati wa mifumo ya unyunyizaji. Wakati huo huo, vijana wengi wameacha kilimo kwa sababu wanataka mapato ya haraka katika sekta ya bodaboda," akasema Waziri wa Kilimo katika kaunti hiyo, Bw Dawson Mzenge. Wakati huo huo, mfereji wa Njoro Kubwa, unaohudumia zaidi ya miradi 10 ya unyunyizaji, haujasafishwa kwa karibu miaka miwili. Hali hiyo imepunguza mtiririko wa maji na kuwaathiri mamia ya wakulima. Katika Kaunti ya Tana River, Miradi ya Unyunyizaji ya Bura na Hola nayo inakabiliwa na changamoto za miundomsingi na upatikanaji wa maji. Bura, iliyoanzishwa mwaka wa 1978, ina eneo lililotengwa la hekta 176,000, lakini ni karibu ekari 12,000 pekee zilizo na miundomsingi bora ya unyunyizaji. Serikali imetumia zaidi ya Sh7 bilioni katika mpango wa kuifufua Bura na kubadilisha mfumo kutoka pampu zinazotumia mafuta ya dizeli hadi mfumo wa maji yanayotiririka kwa nguvu ya mvuto asili. Mamlaka ya Kitaifa ya Unyunyizaji inasema mfereji wa kilomita 26 umekamilika na umeongeza upatikanaji wa maji huku ukipunguza matumizi ya dizeli. Katibu wa wizara kuhusu unyunyizaji, Bw Ephantus Kimotho, alisema mfumo mpya ni hatua muhimu ya mabadiliko. "Mradi unakusudia kuondoa gharama kubwa ya kutegemea mafuta kwa unyunyizaji ili uwezo wa unyunyizaji utumike kikamilifu," alisema alipozuru eneo hilo hivi majuzi. Alisema uwekezaji zaidi katika unyunyizaji utaongeza uzalishaji wa kilimo, kuunda ajira na kuimarisha upatikanaji wa chakula nchini. Maafisa wa Serikali pia wameeleza kuwa kuna ongezeko la wawejezaji binafsi wanaotaka kuwekeza katika miradi ya unyunyizaji. Katika mradi wa Bura, kuna mwekezaji anayehusika katika uzalishaji wa miwa ya mbegu katika eneo la ekari 700. Majaribio hayo yanahusisha aina nane za miwa kwa lengo la kubaini aina zinazofaa zaidi kwa eneo hilo. Serikali inaamini kuwa ubia kama huo unaweza hatimaye kuibadilisha Bura kuwa kitovu cha kilimo na viwanda chenye shughuli nyingi. Huko Kwale, sehemu ya umwagiliaji ya mradi wa Sh20 bilioni wa Bwawa la Mwache ilifutwa baada ya tathmini kuonyesha kuwa gharama za kusukuma maji ingekuwa kubwa na isiyo endelevu. Mradi huo sasa unaelekezwa zaidi kwenye unyunyizaji unaolenga wakulima wadogo karibu 2,000.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 21 Jul 2026 00:55:51

GenZ aibuka na mbinu ya kuzuia wizi wa kura 2027 aliyojaribu katika uchaguzi wa Ol Kalou

UCHAGUZI mdogo wa ubunge wa Ol Kalou ulilipa jukwaa la People's IEBC funzo muhimu kuhusu changamoto za kutumia teknolojia katika kuthibitisha matokeo ya uchaguzi kwa wakati. Jukwaa hilo, linaloendeshwa na vijana wenye ujuzi wa teknolojia, lilifanikiwa kuthibitisha matokeo kutoka vituo 93 kati ya 144 kabla ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kutangaza rasmi mshindi. Hesabu zake zilionyesha mgombea wa DCP Sammy Ngotho akiwa mbele kwa asilimia 85.7 ya kura, akifuatiwa na mgombea wa UDA Samuel Muchina kwa asilimia 12.7. Mwanzilishi wa teknolojia ya People's IEBC, Daniel Miringa, alisema lengo halikuwa kuchukua nafasi ya IEBC bali kuonyesha kuwa wananchi wanaweza kutumia teknolojia kuthibitisha matokeo kwa uwazi. Hata hivyo, mradi huo ulikumbana na changamoto kadhaa. Baadhi ya waangalizi walishindwa kupata Fomu 35A baada ya polisi kutawanya watu kwa vitoza machozi na kuruhusu maafisa wa IEBC na maajenti wa vyama pekee kubaki ndani ya vituo vya kupigia kura. Katika baadhi ya vituo, waangalizi walijiondoa dakika za mwisho kutokana na sababu binafsi, hali iliyolazimisha jukwaa hilo kusubiri IEBC kuchapisha fomu zilizokosekana ili kukamilisha hesabu zake. Bw Miringa alisema ni muhimu kuwa na waangalizi wa akiba katika kila kituo cha kupigia kura ili kuhakikisha shughuli hiyo haiathiriki endapo mmoja atashindwa kutekeleza jukumu lake. "Mbali na changamoto za nyanjani, mfumo huo pia ulikabiliwa na jaribio la udukuzi wa mtandao saa chache kabla ya uchaguzi kuanza. "Kifaa kimoja kilituma zaidi ya maombi 200,000 kwa mfumo huo kwa lengo la kuulemea, lakini wahandisi walizuia majaribio hayo na mfumo ukaendelea kufanya kazi bila hitilafu," akasema Bw Miringa. Kutokana na tukio hilo, jukwaa hilo limeimarisha usalama wa mtandao kwa kuweka vizuizi dhidi ya maombi yasiyo ya kawaida ya udukuzi. Baada ya majaribio ya Ol Kalou, People's IEBC inapanga kushirikiana na mashirika yaliyoidhinishwa ya uangalizi wa uchaguzi kama ELOG pamoja na kutafuta idhini rasmi kutoka kwa IEBC ili waangalizi wake waruhusiwe kubaki vituoni hadi fomu za matokeo zitolewe. "Wananchi wanastahili kuruhusiwa kupakua Fomu 35A moja kwa moja na kusambaza matokeo kupitia majukwaa mbalimbali ya kidijitali badala ya kutegemea TikTok pekee," akaongeza. Kwa mujibu wa Bw Miringa, uchaguzi wa Ol Kalou ulikuwa jaribio la kwanza la mfumo huo na umeonyesha kuwa teknolojia pekee haitoshi kuhakikisha uchaguzi huru na wa uwazi. Alisema mafanikio yanategemea pia maandalizi mazuri, ushirikiano, ulinzi wa mtandao, upatikanaji wa vibali na imani ya wananchi. Aliongeza kuwa mafunzo yaliyopatikana yataisaidia People's IEBC kuboresha mfumo wake kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027 ili wananchi waweze kuthibitisha matokeo ya uchaguzi kwa uwazi zaidi.

read more