T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 11 Jul 2026 01:55:19

Kupata huduma muhimu bado ni changamoto licha ya serikali kuanzisha vitengo vipya vya utawala 2023

LICHA ya serikali kuanzisha vitengo vipya vya utawala nchini tangu mwaka 2023 kwa lengo la kupeleka huduma karibu na wananchi, kuimarisha usalama na kuboresha uratibu wa shughuli za serikali, uchunguzi umebaini baadhi ya vitengo hivyo bado havijaanza kufanya kazi kikamilifu. Sababu kuu zinazochelewesha utekelezaji ni ukosefu wa fedha, kuchelewa kuajiri machifu na manaibu wao, pamoja na ukosefu wa ofisi na miundombinu muhimu. Maeneo yaliyoathirika zaidi ni Kaskazini Mashariki na Bonde la Ufa, ambako vitengo vingi vilianzishwa ili kukabiliana na changamoto za usalama. Katika eneo la Kaskazini Mashariki pekee, angalau tarafa saba, kata 26 na kata ndogo 38 bado havijaanza kutoa huduma. Kaunti ya Wajir inaongoza kwa kuwa na vitengo 40 visivyofanya kazi, ikifuatiwa na Garissa ikiwa na 19 na Mandera 12. Wakazi wanasema changamoto za usalama, migawanyiko ya koo na uhaba wa watumishi zimekwamisha utekelezaji. Garissa kwa mfano, baadhi ya wakazi bado husafiri zaidi ya kilomita 150 kupata huduma muhimu kama vitambulisho vya kitaifa na vyeti vya kuzaliwa. Kamishna wa Kanda ya Kaskazini Mashariki, Bw John Otieno, hata hivyo alisema mchakato unaendelea, akibainisha kuwa machifu na manaibu wao wanaendelea kuajiriwa huku manaibu wa makamishna wa kaunti tayari wakipelekwa katika maeneo mengi mapya. Kaunti ya Turkana imeonyesha mafanikio na changamoto kwa pamoja. Vitengo vipya kama Lokichogio, Aroo, Lokiriama na Suguta vimechangia kuimarisha usalama katika baadhi ya maeneo ya mpakani, ingawa wizi wa mifugo, ukosefu wa magari ya doria na barabara mbovu bado vikitatiza utoaji wa huduma. Katika mpaka wa Kenya na Sudan Kusini, wakazi wanasema hali ya amani imeimarika tangu kuanzishwa kwa vitengo hivyo mwaka 2024, huku kamati za amani na usimamizi wa rasilimali zikisaidia kuzuia migogoro. Katika Kaunti ya Kilifi, Tarafa ya Chasimba ndiyo pekee inayokaribia kuanza kufanya kazi kikamilifu, huku maeneo mengine kama Kitsoeni na Mwakambi yakiwa bado hayana machifu wala ofisi. Hali kama hiyo inashuhudiwa Taita Taveta ambako baadhi ya maeneo yanasubiri maafisa kupelekwa licha ya mahojiano kukamilika. Kaunti za Homa Bay na Kisumu pia zina vitengo vipya ambavyo bado haviwezi kutoa huduma zote za serikali kutokana na ukosefu wa watumishi na miundombinu. Wakazi wengi bado hulazimika kusafiri hadi makao makuu ya kaunti ndogo kupata huduma za usajili wa vitambulisho, vyeti vya kuzaliwa na huduma za polisi. Hata hivyo, Busia, baadhi ya wakazi wanasema vitengo vipya vimepunguza gharama na muda wa kupata huduma za serikali. Lakini katika maeneo jirani ya Mumias West, vituo vipya vya polisi bado havijaanza kufanya kazi licha ya fedha kutumika kujenga miundombinu hiyo. Huko Samburu, zaidi ya miezi sita baada ya kutangazwa kwa kaunti ndogo mpya, utekelezaji bado umekwama kutokana na ukosefu wa fedha.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 11 Jul 2026 00:55:06

Ruto ajipigia debe akizindua awamu ya pili ya mpango wa Nyota

RAIS William Ruto Ijumaa alizindua rasmi awamu ya pili ya mpango wa kuwawezesha wafanyabiashara vijana (NYOTA), katika maeneo mbalimbali nchini kupitia mawaziri na maafisa wengine wakuu. Hatua hiyo ilionyesha mkakati mpya wa serikali wa kutumia mawaziri kufikisha sera na mipango yake moja kwa moja kwa wananchi huku ikipanua utekelezaji wa mpango huo wa kuwawezesha vijana. Rais Ruto aliongoza uzinduzi katika Uwanja wa Michezo wa Ulinzi jijini Nairobi, huku Naibu Rais Kithure Kindiki akiongoza shughuli za kaunti za Nakuru, Baringo na Nyandarua mjini Nakuru. Mkuu wa Mawaziri Waziri, Musalia Mudavadi aliongoza uzinduzi eneo la Magharibi uliohusisha Kakamega, Vihiga, Busia na Bungoma katika Chuo Kikuu cha Masinde Muliro. Naye Waziri wa Utumishi wa Umma, Geoffrey Ruku, aliongoza uzinduzi Meru, Embu na Tharaka Nithi mjini Chuka, huku Waziri wa Ardhi, Alice Wahome, akiongoza shughuli za kaunti za Nyeri, Kirinyaga na Murang'a. Waziri wa Kazi, Alfred Mutua alisimamia uzinduzi Machakos, Makueni na Kitui mjini Kitui. Shughuli kama hizo zilifanyika pia Nanyuki, Kapenguria, Eldoret, Bomet, Malindi, Mombasa, Kisumu, Kisii pamoja na Mandera, Wajir, Garissa na Marsabit. Ingawa alikuwa Nairobi, Rais Ruto alihutubia taifa kupitia matangazo ya moja kwa moja yaliyotangazwa katika vituo vyote vya uzinduzi, jambo lililoruhusu mawaziri na viongozi wengine kuwasilisha ujumbe mmoja wa kitaifa kwa wakati mmoja. Mpango huo unaolenga kuwawezesha vijana unatoa mtaji wa kuanzisha biashara, mafunzo ya ujasiriamali pamoja na ushauri wa kitaalamu ili kuwasaidia vijana kuanzisha na kukuza biashara zinazoweza kuzalisha ajira. Zaidi ya vijana 14,000 kutoka Nairobi, Kiambu na Kajiado walihudhuria uzinduzi huo jijini Nairobi, huku uzinduzi wa wakati mmoja ukiwawezesha vijana kutoka kaunti zote 47 kushiriki bila kulazimika kusafiri umbali mrefu. Serikali ilitenga Sh5.5 bilioni kufadhili vijana 110,000 wenye umri wa kati ya miaka 18 na 29 katika awamu ya kwanza ya mpango huo. Kwa jumla, NYOTA inatarajiwa kuwafikia takriban vijana 820,000 kupitia ufadhili wa biashara, ukuzaji wa ujuzi na fursa za ajira.  "Tunataka kuhakikisha hakuna Mkenya anayeachwa nyuma. Zamani baadhi ya maeneo na wananchi walibaki nyuma, lakini sasa tumedhamiria kila Mkenya ajivunie nchi yake. Ndiyo maana mpango huu unatekelezwa katika wadi zote 1,450 nchini," alisema Rais Ruto. Alisema mpango huo umeundwa ili kuwapa vijana nafasi ya kushiriki katika ukuaji wa uchumi bila kujali kiwango cha elimu, hali ya kijamii au mwelekeo wao wa kisiasa. "Nataka kuwaambia vijana kuwa huu ni mpango wa vijana wenye umri wa miaka 18 hadi 29. Umeundwa kwa ajili ya vijana wa Kenya," alisema. Rais alisema walengwa wakuu ni vijana ambao kwa muda mrefu wamekosa mikopo kutoka taasisi za kifedha kutokana na ukosefu wa dhamana, mtaji au mitandao ya kibiashara. Alisisitiza kuwa uteuzi wa wanufaika utaongozwa na uwazi na uwajibikaji, wala si upendeleo wa kisiasa. "Hauhitaji kuwa gavana, chifu au mtu maarufu ili kufaidika. Mpango huu ni wa uwazi na uwajibikaji, na hautaendeshwa kwa misingi ya upendeleo," alisema. Aliwataka wanufaika kuripoti mtu yeyote atakayewaitisha fedha au kuwaelekeza kuunga mkono chama fulani cha kisiasa ili wapate nafasi katika mpango huo. "Huu si mpango wa kisiasa. Ni mpango wa biashara unaolenga kuwawezesha vijana," alisisitiza. Rais pia alisema hata vijana ambao hawakumaliza masomo ya sekondari au waliosoma hadi darasa la nane watapewa nafasi sawa. "Vijana wote ni Wakenya na serikali yetu ina wajibu wa kuwajali," alisema. Mbali na mtaji, wanufaika watapatiwa mafunzo ya biashara, ushauri na ufuatiliaji wa karibu ili kuhakikisha biashara zao zinakuwa endelevu. Hatutawapa fedha pekee. Tutawafunza, tutawashauri na tutatembea nanyi hadi mfanikiwe," alisema Rais.  Kwa baadhi ya wanufaika, mpango huo tayari umeanza kubadili maisha yao. Kaunti ya Bungoma, Musembe alitumia fedha hizo kufungua duka la vifaa vya kielektroniki baada ya miaka mingi ya kukosa mtaji wa kununua bidhaa. Katika Kakamega, Sonya Wembo aliwekeza fedha hizo katika ufugaji wa kuku, akisema sasa ana nafasi ya kujenga biashara itakayomwezesha kujitegemea. Huko Kitui, Masoso Kituti alifungua bucha na anasema mtaji huo umempa fursa ya kujenga chanzo cha kudumu cha mapato. Garissa, Najma alipanua biashara yake kwa kuongeza bidhaa dukani, huku Kiprono wa Eldoret akiwekeza katika kilimo cha parachichi akisema ni uwekezaji wa muda mrefu utakaomletea kipato cha baadaye. Mbali na uzinduzi wa NYOTA, shughuli za Ijumaa zilionyesha jinsi serikali ya Kenya Kwanza inavyozidi kutumia mawaziri kueneza sera zake kote nchini kwa wakati mmoja badala ya kutegemea ziara za Rais pekee.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Fri, 10 Jul 2026 23:55:27

Wafanyabiashara Keumbu walilia hasara baada ya mkutano wa Linda Mwananchi kuvurugwa

WAFANYABIASHARA katika Soko la Keumbu, Kaunti ya Kisii, wanakabiliwa na wakati mgumu baada ya biashara yao kudorora kufuatia vurugu zilizotokea wakati wa mkutano wa kisiasa wa viongozi wa Linda Mwananchi Ijumaa iliyopita. Hali imezidi kuwa mbaya kutokana na kampeni kwenye mitandao ya kijamii inayowahimiza wananchi kususia bidhaa kutoka sokoni humo, kwa madai kwamba baadhi ya wafanyabiashara walihusika katika vurugu hizo. Ingawa hali ya usalama imeanza kutulia, wafanyabiashara wanasema idadi ya wateja imepungua kwa kiasi kikubwa na wengi wao sasa wanapata hasara. Bi Josephine Mang'ere alisema biashara ilikuwa ikiendelea vizuri kabla ya mkutano huo kuvurugika. "Tulikuwa tumewasubiri viongozi wa Linda Mwananchi, lakini baada ya muda mawe yakaanza kurushwa. Tangu siku hiyo biashara imekuwa ngumu. Tunapoenda kuuza bidhaa zetu watu hawazinunui. Tunaomba tusamehewe," alisema. Kwa upande wake, Bi Sophia Moraa alisema biashara yake ya parachichi imeathirika vibaya kwani wateja wengi wamekataa kununua mazao yake, hali iliyosababisha baadhi yake kuoza. "Sisi ni wafanyabiashara wasio na hatia. Tunapowafuata wateja barabarani wanatuambia tuuze bidhaa zetu kwa viongozi wanaotuhumiwa kusababisha vurugu. Tunataka siasa za amani," alisema. Bi Mary Moraa alisema wafanyabiashara sasa wanahimiza amani na kuheshimiana kisiasa. "Sisi ni wazazi. Kijana aliyefariki ni mtoto wetu pia, na kifo chake kinatuumiza. Wanasiasa wote waruhusiwe kuhutubia wananchi bila ubaguzi," alisema. Wakati huo huo, Meshack Yoge, mmoja wa manusura wa shambulizi dhidi ya msafara wa Linda Mwananchi, alisema anaamini alinusurika kifo kwa bahati. Bw Yoge, ambaye alijeruhiwa jicho baada ya kupigwa na jiwe, alisema tukio hilo lilikuwa la kutisha na bado hajapona kikamilifu. Alisema walikuwa wakielekea Keroka baada ya mkutano wa Kisii mjini na walipofika Keumbu, walivamiwa na kundi la watu waliokuwa wakirusha mawe na kubeba rungu, mishale na pinde. "Tuliona watu wakikimbia kuelekea kwetu wakipiga kelele wakisema, 'Waueni!' Dirisha la gari lilivunjwa, jiwe likanigonga usoni na kujeruhi jicho. Nilinusurika kupoteza jicho na meno," alisema. Aliongeza kuwa walilazimika kukimbia kwa kasi kuokoa maisha yao na baadaye akapelekwa hospitalini Keroka ambako alipatiwa matibabu. Mgombeaji wa udiwani wa Kisii Central, Bw Andrew Moindi Mochache, aliyekuwa ndani ya gari hilo, alisema waliona kifo wazi. "Niliona kifo kwa macho yangu. Watu waliotushambulia walikuwa wamekusudia kutuua," alisema. Kiongozi wa People's Liberation Party (PLP) Martha Karua na Mbunge wa North Mugirango Joash Nyamoko walilaani vurugu hizo, wakisisitiza kuwa siasa zinapaswa kuendeshwa kwa amani. Bi Karua alisema hakuna anayepaswa kuzuiwa kutoa maoni yake au kushiriki shughuli za kisiasa kwa amani, huku Bw Nyamoko akiwataka vijana kuepuka kutumiwa na wanasiasa kuchochea ghasia.

read more