T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Wed, 08 Jul 2026 21:55:27

Kunanyesha pesa na miradi Ol Kalou uchaguzi mdogo ukiweka historia kuwa ghali zaidi

HUKU zikiwa zimesalia siku nane kabla ya uchaguzi mdogo wa eneobunge la Ol Kalou utakaofanyika Julai 16, eneo hilo linashuhudia kampeni zinazotajwa kuwa miongoni mwa ghali zaidi katika historia ya Kaunti ya Nyandarua. Vyama vya United Democratic Alliance (UDA) na Democracy for the Citizens Party (DCP) vinaongoza kampeni hizo kwa kutumia mikakati mbalimbali ya kuwashawishi wapigakura. Mbali na mikutano ya kisiasa, wagombeaji na wafuasi wao wamekuwa wakigawa fedha, zawadi na kuandaa mikutano ya uhamasishaji huku serikali ikiendelea kuzindua miradi ya maendeleo katika eneo hilo. Kiti hicho kilibaki wazi baada ya kifo cha Mbunge Njuguna Kiaraho wa chama cha Jubilee, Machi 29, 2026. Wanaowania kiti hicho ni Kamau Ngotho wa DCP, Muchina Nyaga wa UDA, Wilson Kigwa wa Jubilee, Rachel Wangui wa People's Democratic Party, Mathenge Mwaniki wa Kenya Moja Movement, Abdifatah Hussein wa Federal Party of Kenya, Timothy Kamau wa People's Renaissance Party, Stephen Wanyoike wa National Liberal Party na Edwin Muchiri wa Party of National Unity. Kwa mujibu wa walio karibu na kampeni za DCP, makazi ya Seneta wa Nyandarua John Methu katika eneo la Mugumo yamegeuzwa kuwa kituo kikuu cha uratibu wa shughuli za chama hicho. [caption id="attachment_189921" align="alignnone" width="720"] Wakazi waliohudhuria mkutano wa kisiasa wapewa magodoro. Picha|Hisani[/caption] Kila asubuhi, makundi mbalimbali hukusanyika hapo kabla ya kutumwa katika maeneo tofauti kufanya kampeni. Washiriki hupewa kifungua kinywa na fedha za kujikimu zinazokadiriwa kuwa kati ya Sh500 na Sh1,000 kabla ya kuanza shughuli za siku. Akizungumza jana, kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua aliwataka wakazi wa Ol Kalou kutodanganywa na miradi ya maendeleo inayotekelezwa na serikali wakati huu wa kampeni. "Serikali inaweza kuleta hata boti, transfoma, treni za kasi, matangi ya maji pamoja na miradi mingine ambayo haijawahi kufikishwa Ol Kalou tangu 1963. Msikubali kuuza haki yenu ya kupiga kura kwa sababu ya zawadi za dakika za mwisho," alisema Bw Gachagua. Kwa upande wa UDA, kampeni zinaonekana kuwa na mtandao mpana zaidi. Chama hicho kimeunda timu mbalimbali zinazolenga makundi tofauti ya wapigakura huku washiriki wakipewa fedha za kujikimu kulingana na aina ya shughuli wanazoshiriki. Baadhi ya timu hizo husafirishwa hadi miji jirani kama Gilgil kwa mikutano ya kupanga mikakati, ambapo kila mshiriki hudaiwa kulipwa kati ya Sh1,000 na Sh2,000. Duru zenye ufahamu kuhusu kampeni hizo zinaeleza kuwa UDA huandaa wastani wa mikutano sita kila siku, huku viongozi wa serikali na waliochaguliwa wakihusika moja kwa moja katika shughuli hizo. Mbali na mikutano ya hadhara, chama hicho pia kimekuwa kikifanya mikutano na viongozi wa dini, wazee wa makanisa na waumini wenye ushawishi mkubwa, mikutano ambayo huwasilishwa kama warsha za amani na elimu ya uraia. Kiongozi mmoja wa kidini aliyeshiriki katika baadhi ya mikutano hiyo alisema kiwango cha fedha kinachotolewa hutegemea hadhi ya mkutano. Alidai kuwa mikutano ya kiwango cha kaunti washiriki hupokea takriban Sh5,000 kila mmoja huku mikutano ya ngazi ya mashinani wakipata karibu Sh3,000, bila kujumuisha fedha zinazotolewa kwa makanisa na viongozi wa dini wanaoratibu shughuli hizo. Kwa mujibu wa watu wanaofahamu mipango ya kampeni, mikutano mingi ya ndani huvutia takriban watu 500 wanaopewa kati ya Sh1,000 na Sh2,000 kila mmoja. Wanaoongoza kampeni pia hulipwa kati ya Sh5,000 na Sh10,000. Makadirio yanaonyesha kuwa UDA inaweza kutumia zaidi ya Sh3 milioni kwa siku kugharamia mikutano ya ndani pekee, bila kujumuisha gharama za usafiri, malazi, chakula na shughuli nyingine za kampeni. Baada ya mikutano ya hadhara, washiriki wengi huripotiwa kupanga foleni katika makundi ya watu kumi, utaratibu unaojulikana kama "ikumi ikumi", ambapo kila mmoja hupokea kati ya Sh300 na Sh500. Kutumiwa kwa fedha kumeibua biashara mpya kwa baadhi ya vijana wa eneo hilo. Makundi ya vijana hukodisha pikipiki kwa siku nzima na kuhama kutoka mkutano mmoja wa kampeni hadi mwingine ili kuongeza kiwango cha fedha wanachopata. Mwendesha bodaboda James Kanja alisema vijana watatu au wanne huchangia takriban Sh3,000 kukodisha pikipiki kwa siku pamoja na gharama ya mafuta. "Ni biashara nzuri kuliko kusubiri abiria mjini. Tunaweza kuhudhuria zaidi ya mikutano mitano kwa siku na kila mmoja akaondoka na kati ya Sh2,500 na Sh4,000," alisema. Mwendesha bodaboda mwingine, Robert Kiambati, alisema vijana hufuatilia ratiba za kampeni ili kujua mikutano inayotarajiwa kutoa fedha nyingi zaidi. Huku kampeni zikiendelea, serikali nayo imeongeza kasi ya kuzindua miradi ya maendeleo katika eneo hilo. Miradi hiyo ni pamoja na usambazaji wa mitungi 20,000 ya gesi, matangi ya maji, godoro, vyakula, vifaa vya kidijitali kwa shule za sekondari msingi, pamoja na boti mbili za thamani ya Sh5 milioni kwa Bwawa la Gwa Kiongo. Mawaziri na Makatibu mbalimbali wamekuwa wakizuru eneo hilo mara kwa mara kuzindua miradi ya barabara, umeme, nyumba za bei nafuu, masoko ya kisasa, reli na huduma za kidijitali. Kwa upande wa DCP, uchaguzi huo pia umegeuka kuwa uwanja wa kujitambulisha kwa wanasiasa wanaojiandaa kugombea viti mbalimbali katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2027. Baadhi ya wanaotaka ugavana, ubunge na uwakilishi wa wadi wamekuwa wakifanya kampeni za nyumba kwa nyumba kwa gharama zao wenyewe ili kuongeza nafasi za mgombeaji wa DCP, Kamau Ngotho.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Wed, 08 Jul 2026 11:18:55

Wakazi Mbeere walia kuondolewa transfoma 'baada ya kura'

WAKAZI wa eneo bunge la Mbeere North, Kaunti ya Embu, wamelalamikia kuondolewa kwa transfoma za umeme miezi minane tu baada ya serikali kuwaunganishia umeme kupitia mpango wa Last Mile Connectivity na Stima Mashinani. Wakazi hao wanasema walipata umeme kwa mara ya kwanza wakati wa uchaguzi mdogo wa Novemba 27, 2025, lakini sasa wanahofia kurejea gizani baada ya Kampuni ya Kusambaza Stima Kenya (KPLC) kuanza kuondoa transfoma bila maelezo ya kina. Faith Kithaka wa kijiji cha Muramba asema maafisa wa KPLC waliondoa transfoma katika eneo lao wiki mbili zilizopita na hawajairejesha. Wakazi wanasema kuondolewa kwa transfoma hizo kumekatiza shughuli zao za kila siku na kuwarudisha katika maisha ya kutumia mishumaa na taa za mafuta. "Tuliishi gizani kwa miaka mingi. Serikali ilituunganishia umeme wakati wa uchaguzi mdogo, lakini kabla hatujafaidika kikamilifu, transfoma zimeondolewa," alisema Bi Kithaka. Katika kijiji cha Njarange, hali ilikuwa sawa huku wakazi wakishuhudia maafisa wa KPLC wakiondoa transfoma nyingine. Julius Njeru wa kijiji cha Rwanjeru alisema kukosekana kwa umeme kumeathiri biashara na masomo ya watoto. "Biashara zimeathirika na watoto hawawezi kusoma usiku kwa sababu stima zimekatika," alisema. Baadhi ya wakazi walikumbuka jinsi viongozi wa serikali na wanasiasa wa chama cha UDA walivyozunguka eneo hilo wakati wa uchaguzi mdogo wakiahidi maendeleo iwapo wangemuunga mkono mgombea wa chama hicho. "Tuliwapigia kura na tukaletewa umeme. Sasa miezi michache baadaye wanaondoa transfoma. Hii si haki," alisema mkazi mmoja. Wengine walidai kuwa transfoma hizo zinapelekwa Ol Kalou, ambako kutafanyika uchaguzi mdogo Julai 16, ili kuvutia wapigakura. Wakazi walitishia kuandamana iwapo vifaa hivyo havitarejeshwa haraka. Hata hivyo, Mbunge wa Mbeere North, Leo Wamuthende, alipuuza madai hayo akisema baadhi ya watu wanapotosha umma kwa maslahi ya kisiasa. "Nimeona taarifa zinazodai serikali inaondoa transfoma katika Mbeere North. Madai hayo si ya kweli na yanalenga kupotosha wananchi," alisema. Alifafanua kuwa KPLC inaendesha mpango wa kawaida wa kukarabati transfoma, hasa zile za zamani, ili kuboresha uthabiti wa huduma ya umeme. Meneja wa KPLC Kaunti ya Embu Vincent Okello, pia alikanusha madai kuwa transfoma hizo zinapelekwa Ol Kalou kwa sababu za kisiasa. Alisema kampuni hiyo "haijihusishi na siasa" na kueleza kuwa baadhi ya transfoma ziliharibiwa na wahalifu huku nyingine zikiharibika kutokana na hitilafu za kiufundi. "Katika Mbeere North na Runyenjes, transfoma tatu ziliharibiwa na ziliondolewa kupelekwa Nairobi kutengenezwa," alisema. Hata hivyo, baadhi ya wakazi walitilia shaka maelezo hayo wakisema baadhi ya transfoma zilizoondolewa ni mpya na hazikuwa na hitilafu zozote. "Transfoma hazikuharibiwa wala kuvurugwa. Tunataka tuambiwe ukweli kuhusu zilikopelekwa," alisema mkazi mwingine.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Wed, 08 Jul 2026 10:12:38

Chama cha Uanahabari chawasha taa ya vipaji Kairi Boys

CHAMA cha Uanahabari katika Shule ya Upili ya Kairi Boys, Gatundu Kaskazini, Kaunti ya Kiambu, kinaendelea kuwa chombo muhimu cha kuwakuza wanafunzi kitaaluma na kitalanta huku kikiwafungulia milango katika fani zinazohusiana na lugha na mawasiliano. Pamoja na kukuza vipaji vya wanafunzi katika sanaa hizo anuwai, chama hicho pia kinawapa msukumo wa kujitosa katika ualimu, tafsiri, upigaji picha na uhariri wa vitabu, video na filamu. Isitoshe, kinalenga kuimarisha umilisi wa Kiswahili na Kiingereza ili kuwajenga wanafunzi wenye uwezo wa kujieleza kwa ufasaha kimazungumzo na kimaandishi. [caption id="attachment_189899" align="alignnone" width="2560"] Baadhi ya walimu wa Shule ya Upili ya Kairi Boys iliyoko Gatundu Kakazini, Kaunti ya Kiambu, walipojumuika kwa picha ya pamoja.[/caption] Wanachama hukutana baada ya vipindi vya masomo mchana kutwa ili kujadili mikakati ya kuendeleza chama na kukipa nguvu zaidi. Aidha, chama kinatarajia kuanzisha kitengo cha uigizaji na kuzindua jarida rasmi la shule mwaka ujao, hatua itakayowapa wanafunzi jukwaa maridhawa la kuonyesha ubunifu wao katika uandishi na sanaa nyinginezo. Mafanikio ya chama tayari yanaonekana. Wanafunzi wanaoshiriki shughuli zake kikamilifu wamekuwa wakifaulu vyema katika mitihani ya Kiswahili na Kiingereza huku wakionyesha kujiamini zaidi katika mawasiliano na shughuli tofauti za shule. Mlezi wa chama, Bi Doreen Kathurima, anaungama kuwa chama hicho kimechangia pakubwa maendeleo ya wanafunzi na kimekuwa chanzo cha mabadiliko muhimu shuleni. "Mbali na kupiga jeki shughuli za Idara ya Lugha, chama hiki kinakuza maadili na kuboresha matokeo ya KCSE. Pia tumeshuhudia maendeleo makubwa katika ulumbi, utunzi wa mashairi na utangazaji wa habari miongoni mwa wanachama," anaeleza. [caption id="attachment_189900" align="alignnone" width="2560"] Wanafunzi wa Shule ya Upili ya Kairi Boys wakifuatilia kwa makini matukio na mawasilisho mbalimbali wakati wa hafla ya kielimu waliyoiandaa. PICHA ZOTE | RICHARD MAOSI[/caption] Mwalimu Mkuu, Bw Anthony Mwaria, anakiri kuwa chama hicho kinawaandaa wanafunzi kwa ajili ya maisha ya baadaye. "Chama hiki ni jukwaa linaloamsha hamu ya wanafunzi kujitosa katika ulingo wa uanahabari na taaluma nyingine zinazofungamana na lugha. Vilevile kinawalea na kuwakuza ipasavyo ili wawe watafiti na waandishi wabunifu wenye uwezo wa kushindana kimataifa," anasema. Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Ushauri Nasaha, Bi Norah Biyaki, anasisitiza kuwa nidhamu na kujituma kwa wanafunzi ni msingi wa mafanikio ya chama. "Tunawahimiza wanafunzi kuwa na ari ya kujifunza, nidhamu ya hali ya juu na moyo wa kujituma ili waweze kufaidika kikamilifu na fursa tofauti zinazotolewa na chama hiki," akasema Bi Biyaki katika kauli inayotiliwa mkazo na Naibu Mwalimu Mkuu, Bw Michael Ngari. Kupitia shughuli zake, Chama cha Uanahabari shuleni Kairi Boys kinaendelea kuwajenga wanafunzi kuwa wataalamu, viongozi na wasanii wa kesho.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Wed, 08 Jul 2026 10:30:12

Misri wafokea Fifa kwa 'ukora' katika mechi dhidi yao na Argentina

KOCHA wa Misri Hossam Hassan amesema hana nia ya kutazama mechi zilizosalia za Kombe la Dunia akisema refa alichangia timu hiyo kubanduliwa na Argentina mnamo Jumanne usiku. Katika mechi nyingine, Uswizi walibandua Colombia 4-3 kupitia mikwaju ya penalti na kufuzu robo fainali. Timu hizo zilikuwa zimeagana sare tasa muda wa kawaida na ule wa ziada kabla ya kuamuliwa na mikwaju ya penalti. Sasa Argentina na Uswizi zitachuana katika robo fainali wikendi hii huku Misri na Colombia zikiaga kombe. Misri walikuwa wakiongoza 2-0 zikiwa zimesalia dakika 11 mechi iishe katika raundi ya 16 dhidi ya Argentina. Kwa masikitiko walifungwa mabao matatu na ikabidi waage mashindano hayo ya hadhi ya soka. [caption id="attachment_189904" align="alignnone" width="2560"] Mshambuliaji nyota wa Argentina Lionel Messi ashangilia kufunga bao la kusawazisha dhidi ya Misri katika mechi ya 16-bora uga wa Atlanta, jimbo la Georgia, Amerika, Julai 7, 2026. Argentina ilishinda mechi 3-2. Picha|Reuters[/caption] Mkongwe Lionel Messi aling'ara katika mechi hiyo na kutumia uweledi wake kuhakikisha Argentina inatinga robo fainali. Hassan alilalamika kuwa walionewa na hana nia ya kutazama mechi zilizosalia za kombe la dunia. "Naenda nyumbani na sitatazama mechi hizo kwa sababu kilichotutendekea si haki. Tulistahili kupewa penalti, bao letu lilikataliwa na sijui kwa nini lilikataliwa," akasema akionekana mwenye hasira. Egypt walifunga bao dakika ya 62 kupitia Mostafa Zico lakini VAR iliangalia na kutambua kuwa kulikuwa na mpira wa ikabu kwa Argentina kuelekea kufungwa kwa bao hilo. Pia Misri walilia kwamba walistahili kupewa penalti baada ya Hamdy Fathy kuangushwa ndani ya kijisanduku. Hasira yao ilipanda kwa kuwa baada ya tukio hilo kwa kuwa Argentina waliendelea kucheza na kufunga bao dakika ya 92 kupitia Messi. "Mimi huwa sipendi kushindwa na kama kupoteza kwangu kumechangiwa na refa jinsi ilivyofanyika hivi leo, nawaambia tu mashabiki wetu wasikasirike. Tulicheza vizuri sana na kushindwa kwetu kumechangiwa na refa," akaongeza. Hassan alisema alifurahi kuwa wachezaji wake walifuata mwongozo wake mchezoni na waliwalemea Argentina. Misri wamekuwa wakitumia mbinu ya kulinda ngome yao mchezoni lakini dhidi ya Argentina walikuwa wakivamia hasa kupitia mipira mirefu na pia pembeni. Pia mnyakaji wao Mostafa Shoubir alionyesha uweledi wa juu baada ya kuokoa mikwaju hatari ya Argentina. "Najivunia sana wachezaji wangu kwa sababu wengi wao wanacheza kwenye Ligi Kuu ya Misri nao wapinzani wetu walikuwa na wachezaji wanaoshiriki ligi za kifahari za Ulaya," akaongeza. Colombia nao watajilaumu wenyewe baada ya nyota wa Bayern Luis Diaz na wenzake kukosa nafasi kadhaa za kufunga na kumaliza mchezo mapema. Kipa wa Uswizi Gregor Kobela aliokoa penalti ya Cucho Hernandez baada ya ile ya Davinso Sanchez kugonga mtambapanya kwa Columbia. Manuel Akanji pia alikosa penalti kwa upande wa Uswisi.

read more