T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 20 Jul 2026 21:55:13

Wahuni wa wakubwa? Hakuna aliyekamatwa kwa ghasia Ol Kalou licha ya ufichuzi

ZAIDI ya siku nne baada ya ghasia zilizoshuhidiwa katika uchaguzi mdogo wa ubunge wa Ol Kalou, hakuna mwanasiasa, mfadhili au mmiliki wa magari yanayodaiwa kutumiwa na watu wenye silaha walioficha nyuso zao ambaye amekamatwa au kuhojiwa. Hali hii imezua maswali kuhusu iwapo wanasiasa wanaochochea vurugu wako juu ya sheria licha ya visa vya uhuni kushuhudiwa peupe. Siku ya uchaguzi, Julai 16, maelfu ya wapigakura walikumbana na kundi la wanaume waliovalia barakoa waliokuwa wakizunguka kwa magari ya kifahari, wakifyatua risasi hewani, kurusha vitoza machozi na kuwashambulia wapigakura, wanahabari na hata baadhi ya maafisa wa polisi. Uchunguzi uliofichua yaliyotokea unaonyesha magari hayo yalikuwa na nambari za usajili zinazozua utata. Miongoni mwao ni Toyota Land Cruiser yenye nambari KDL 477Q, ambayo rekodi za Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi na Usalama Barabarani (NTSA) zinaonyesha imesajiliwa kwa jina la John Njuguna Wanjiku, jina ambalo ni sawa na la Mbunge wa Kiambaa anayejulikana kama Ka-Wanjiku. Mbunge huyo alikiri kuwa gari lake lilikuwa Ol Kalou lakini akakanusha kuhusika katika vurugu zozote za uchaguzi. Aidha, gari jingine lililotumiwa na watu hao lilikuwa na nambari KDW 600Q, ilhali rekodi za NTSA zinaonyesha nambari hiyo imesajiliwa kwa gari aina ya Toyota Probox linalomilikiwa na kampuni ya Vipingo Industries. Kampuni hiyo ilisema haina Land Cruiser nyeusi, hali inayoashiria matumizi ya nambari bandia. Licha ya ushahidi huo na video zilizosambaa zikionyesha vurugu, polisi walikuwa bado hawajawahoji wamiliki wa magari hayo wala watu waliorekodiwa wakihusishwa na utoaji rushwa na makosa mengine ya uchaguzi. Uchunguzi wa Idara ya Upelelezi nchini (DCI) pia unaonekana kukwama. Kikosi maalumu kutoka makao makuu ya DCI Nairobi kilikuwa bado hakijaanza kazi rasmi huku kikisubiri malalamishi yaandikwe na waathiriwa. Duru kutoka DCI zilisema wachunguzi wanahitaji kwanza kupata taarifa zilizonakiliwa katika vituo vya polisi kabla ya kuwaita walalamishi kutoa ushahidi. Maafisa hao pia wanatarajiwa kuchunguza maandalizi ya kiusalama yaliyowekwa kabla ya uchaguzi huo mdogo. Kabla ya upigaji kura, Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja alikuwa ametangaza kuwa zaidi ya maafisa 1,000 walikuwa wametumwa Ol Kalou kuimarisha usalama. Wachunguzi wanatarajiwa kukagua taarifa za kijasusi, picha za kamera za CCTV na mienendo ya magari yaliyonaswa kwenye kamera yakizunguka eneo hilo ili kubaini waliohusika. Kampeni za uchaguzi huo mdogo pia ziligubikwa na ghasia huku upinzani na serikali wakirushiana lawama. Mnamo Julai 12, lori la kampeni la mgombea wa DCP lilivamiwa na kuchomwa moto katika eneo la Chokereria na watu waliokuwa na silaha. Mkazi wa Ol Kalou, John Kuria, alisema yeye ni mmoja wa walionusurika katika kisa hicho. "Walikuwa wamejihami kwa bunduki na waliturushia vitoza machozi kabla ya kutushambulia. Tunataka waliohusika wakamatwe na kufikishwa mahakamani," akasema Bw Kuria. Siku moja kabla ya uchaguzi, gari la Mbunge wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Kanini Kega pia lilivamiwa, huku polisi wakipata risasi iliyotumika katika eneo la tukio. Wanahabari nao hawakusazwa. Katika kituo cha kupiga kura cha Shule ya Msingi ya AC, watu sita waliokuwa wamevaa barakoa waliwashambulia wanahabari wa kampuni ya Nation Media Group (NMG) na kuwaibia vifaa vya kazi. Mpigapicha wa NTV, George Kieru alipokonywa kamera na kupigwa, huku mwandishi Fabiola Akinyi akinyang'anywa simu kwa kutishiwa bunduki. "Walifika kwa magari ya kifahari, wakaanza kutushambulia na kulazimisha George kufuta picha kabla ya kumpora kamera," alisema Mhariri wa NMG Kanda ya Kusini mwa Bonde la Ufa Brygettes Ngana. Bw Kieru alisema alipigwa hadi kujeruhiwa mkono na mgongo, huku Bi Akinyi akieleza kuwa alielekezewa bunduki tumboni kabla ya kuporwa simu yake. Mpiga picha wa gazeti la Star Enos Teche pia alivamiwa na kuibiwa kamera alipokuwa akirekodi ghasia karibu na Shule ya Msingi ya St Joseph's Catholic. Mkurugenzi wa DCI, Amin Mohamed alisema uchunguzi utawalenga waliotekeleza uvamizi na waliopanga, kufadhili na kuchochea vurugu hizo. Kwa upande wake, Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen amesema hakuna atakayesazwa iwapo atapatikana na hatia, iwe ni mwanasiasa, afisa wa usalama au mtumishi wa serikali. Hata hivyo, viongozi wa dini, asasi za kiraia, vyombo vya habari na wanasiasa wa upinzani wanasema hatua hizo zitakuwa na maana tu ikiwa waliohusika watafikishwa mahakamani. Kiongozi wa DP Justin Muturi alionya kuwa vurugu za Ol Kalou zinaweka msingi hatari kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027. Licha ya mazingira hayo ya hofu na vitisho, mgombea wa DCP Sammy Kamau alishinda uchaguzi huo kwa kura 35,440, akimshinda mgombea wa UDA Samuel Nyagah, aliyepata kura 5,450. Sasa macho yote yanaelekezwa kwa DCI kuona kama uchunguzi huo utawagusa waliohusika kupanga na kufadhili ghasia hizo au utaishia kwa wavamizi wa kawaida pekee.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 20 Jul 2026 14:40:20

Afrika yatakiwa kuwekeza zaidi kwenye ubunifu wa kilimo

AFRIKA inapaswa kuendelea kuwekeza katika ubunifu wa kilimo na kuharakisha matumizi ya teknolojia zilizothibitishwa ili kuongeza kiwango cha uzalishaji wa chakula, kupunguza uagizaji wa vyakula kutoka nje na kujenga mifumo imara ya chakula inayostahimili athari za mabadiliko ya tabianchi. Wito huo ulitolewa wakati wa mkutano wa Harvesting the Future Africa Summit uliofanyika Nairobi mwezi Juni mwaka huu, 2026, ambapo viongozi wa serikali, taasisi za utafiti, sekta binafsi, mashirika ya maendeleo na wafadhili walisisitiza umuhimu wa kupeleka teknolojia zilizofanikiwa kwa wakulima wengi badala ya kusalia katika hatua ya utafiti. Mkutano huo uliandaliwa na Kituo cha Kimataifa cha Uboreshaji wa Mahindi na Ngano (CIMMYT) pamoja na washirika wake wakati ambapo sekta ya kilimo barani Afrika inakabiliwa na ukame wa muda mrefu, gharama za juu za uzalishaji, changamoto za upatikanaji wa mbolea, migogoro na kuyumba kwa uchumi. Mkurugenzi Mkuu wa CIMMYT, Bram Govaerts, alisema lengo ni kuhakikisha ubunifu wa kilimo unachangia usalama wa chakula, ajira na ukuaji wa uchumi. "Teknolojia zilizofanikiwa zinapaswa kuwafikia wakulima wengi na kwa haraka zaidi," akasema. [caption id="attachment_190349" align="aligncenter" width="300"] Mtambo wa kuosha maparachichi kwenye kiwanda. Picha|Sammy Waweru[/caption] Naye Dkt Agnes Kalibata, mwanachama wa Bodi ya CIMMYT, alisema Afrika tayari ina mifano mingi inayoonyesha jinsi sayansi inavyoweza kuongeza uzalishaji wa kilimo, lakini wadau wanahitaji kupewa raslimali za kutosha ili kufanikisha juhudi hizo. "Kinachohitajika zaidi ni raslimali kuonyesha sayansi na teknolojia zinafanya kazi," Agnes akapendekeza. Washiriki wa mkutano huo wa Harvesting the Future Africa Summit walitaja mbegu bora, mbinu za kilimo himilivu kwa tabianchi, teknolojia za kuboresha afya ya udongo, huduma za ushauri wa kidijitali na mifumo bora ya mbegu kuwa miongoni mwa ubunifu unaowasaidia wakulima kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi huku wakiongeza mavuno na mapato. Aidha, walieleza kuwa kuimarisha sekta ya kilimo kutasaidia kuzalisha ajira, kupunguza utegemezi wa uagizaji wa chakula na kukuza uchumi wa nchi za Afrika. Ripoti ya hivi majuzi ya uchambuzi wa mifumo ya chakula inaonyesha Kenya inakabiliwa na upungufu wa mayai bilioni tano, lita bilioni 6.5 hadi 7.5 za maziwa, tani 340,000 za samaki na tani 5,500 za asali kila mwaka. [caption id="attachment_190350" align="aligncenter" width="300"] Avokado kwenye kiwanda. Picha|Sammy Waweru[/caption] Ripoti hiyo iliyofadhiliwa na Financial Sector Deepening Kenya (FSD Kenya) chini ya mradi wa Green Finance for Youth Employment (GFYE) na kutolewa Mei 2026, inadokeza kuwa Kenya hutumia kati ya Sh288 bilioni na Sh500 bilioni kuagiza chakula kutoka nje kila mwaka. CIMMYT inasisitiza kuwa ushirikiano kati ya serikali, taasisi za utafiti, kampuni za mbegu, mashirika ya wakulima na washirika wa maendeleo ni muhimu ili kuhakikisha teknolojia zinazobuniwa zinawafikia wakulima na kuongeza uzalishaji wa chakula barani Afrika.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 20 Jul 2026 13:46:00

Teknolojia nafuu ziwafikie wakulima

WABUNIFU wa teknolojia za kilimo na mabadiliko ya tabianchi wamehimizwa kuibuka na bunifu faafu, rahisi kutumia na endelevu zinazokidhi mahitaji ya wakulima wa mashamba madogo. Wakulima wa mashamba madogo wanakadiriwa huzalisha zaidi ya asilimia 75 ya chakula nchini Kenya. Mkurugenzi Mkuu wa KickStart International, Peter Juma, anasema wakulima hawakubali teknolojia kwa sababu ni mpya, bali kwa kuwa zinatatua changamoto halisi, zinapatikana kwa gharama nafuu na huwaletea faida. "Teknolojia hukubalika ikiwa ni nafuu – kifedha, inatatua tatizo halisi na inajilipa yenyewe," alisema. Alisema hayo majuzi wakati wa kongamano la Kenya Editors Guild (KEG) Press Club jijini Nairobi, lililowaleta pamoja wanahabari wa kilimo, wahariri, watafiti, wabunifu, watunga sera, wakulima na wadau wengine kujadili namna ya kujenga kilimo kinachostahimili athari za mabadiliko ya tabianchi. [caption id="attachment_190344" align="aligncenter" width="300"] Apu ya kuuza chakula na bidhaa za shambani. Picha|Sammy Waweru[/caption] Juma alisema licha ya juhudi za kuhimiza matumizi ya teknolojia za kidijitali katika kilimo, wakulima wengi bado wanahitaji teknolojia rahisi kutumia, kutunza na kumudu. "Teknolojia zinapaswa pia kuzingatia mahitaji ya wanawake kwa kuwa nyepesi na zinazobebeka kwa urahisi," alielezea. Alitaja pampu za maji zinazotumia nishati ya jua na mashine za kilimo kuwa miongoni mwa teknolojia ambazo bado ni ghali kwa wakulima wengi. Kwa mfano, alisema pampu za maji huuzwa kati ya Sh40,000 na Sh200,000, hali inayozifanya zisifikie wakulima wengi wa mashamba madogo. Juma aliwataka wabunifu kuzingatia uwezo wa wakulima kifedha, ili teknolojia wanazobuni ziweze kuwasaidia kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Washiriki wa kongamano la Kenya Editors Guild (KEG) Press Club walikubaliana kuwa Kenya haina upungufu wa utafiti, kukosa takwimu za tabianchi wala suluhisho za kilimo. [caption id="attachment_190345" align="aligncenter" width="300"] Maji yaliyopampiwa. Pampu za maji zinazotumia nishati ya jua na mashine za kilimo zinatajwa kuwa miongoni mwa teknolojia ambazo bado ni ghali kwa wakulima wengi. Picha|Sammy Waweru[/caption] Changamoto kubwa, walitaja ni kuhakikisha maarifa hayo yanageuzwa kuwa hatua zinazotekelezeka na zinazoweza kutumiwa kwa urahisi na wakulima. Mwanachama wa Baraza Kuu la Kenya Editors Guild, Agnes Mwangangi, alisema wanahabari wana jukumu kueleza simulizi za athari na suluhisho za mabadiliko ya tabianchi, kuwawajibisha viongozi na kusaidia wananchi kuelewa masuala hayo. "Vijana, kwa mfano, wanaongoza katika ubunifu wa teknolojia za kilimo na ujuzi wao wa kidijitali unapaswa kutumiwa kuimarisha usalama wa chakula na kupunguza njaa nchini," Agnes alihimiza.

read more