T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 19 Jul 2026 23:55:59

Raha tele walimu wakiongezwa mshahara mwezi huu

WALIMU nchini wataanza kupokea nyongeza ya mishahara kuanzia malipo ya mwezi huu baada ya Tume ya Kuwaajiri Walimu (TSC) kutekeleza awamu ya pili ya Mkataba wa Makubaliano (CBA) wa miaka ya 2025–2029. Marekebisho hayo ya mishahara, yaliyoanza kutumika Julai 1, 2026, yatawaongezea walimu pesa ya hadi Sh2,055 kwa mwezi kulingana na daraja lao la kazi. Walimu wa madaraja ya C2 na C3 ndio watanufaika zaidi, huku Walimu wa Sekondari I katika daraja la C3 wakipata nyongeza ya juu zaidi. Kupitia barua ya Julai 16, TSC iliagiza wakurugenzi wa elimu wa maeneo yote kuhakikisha viwango vipya vya mishahara vinaanza kutekelezwa mara moja hadi Juni 30, 2027. Mkataba huo ni awamu ya pili ya makubaliano yaliyotiwa saini kati ya TSC na vyama vya walimu vya KNUT, KUPPET na KUSNET. Walimu wataendelea kubaki katika madaraja yao ya sasa lakini watahamishiwa viwango vipya vya mishahara. Walimu ambao nyongeza yao ya kawaida ya kila mwaka huanza Julai 1 watapokea kwanza nyongeza hiyo kabla ya kuhamishiwa kwenye viwango vipya. TSC ilisema walimu wote waliokuwa kazini kufikia Julai 1, 2026 watanufaika na mabadiliko hayo isipokuwa walimu wa mafunzo kwa vitendo (interns). Aidha, tarehe zao za nyongeza za kila mwaka zitaendelea kubaki kama zilivyokuwa. Chini ya viwango vipya, Wakuu Wakuu wa Shule katika daraja la D5 sasa watapokea mshahara wa kati ya Sh133,351 na Sh164,977 kwa mwezi. Wakuu wa Shule waandamizi na Maafisa Wakuu wa Usaidizi wa Mtaala wa daraja la D4 watapata kati ya Sh120,016 na Sh148,480, huku Wakuu wa Shule na Naibu Wakuu wa daraja la D3 wakilipwa kati ya Sh107,634 na Sh131,405. Walimu wa daraja la D2, wakiwemo Naibu Wakuu wa Shule II na Walimu Wakuu waandamizi, watapokea kati ya Sh93,883 na Sh114,322 kwa mwezi, huku walimu wa daraja la D1 pia wakinufaika na viwango hivyo vipya. TSC ilieleza kuwa posho zote zinazolipwa kwa sasa zitaendelea bila mabadiliko. Hizo ni pamoja na posho ya nyumba, mazingira magumu, usafiri, mizigo, likizo ya kila mwaka na posho ya mwongozo kwa walimu wenye ulemavu pale inapohusika. Naibu Katibu Mkuu wa KNUT, Hesbon Otieno, alipongeza hatua hiyo lakini akasema chama hicho kitapigania kipindi kifupi zaidi cha CBA ili walimu waweze kujadiliana kuhusu mishahara na maslahi yao mara kwa mara. Aliongeza kuwa ingawa nyongeza hiyo italeta afueni kwa walimu, haitoshi kukabiliana kikamilifu na changamoto zinazowakabili, zikiwemo gharama ya juu ya maisha, uhaba wa walimu, kucheleweshwa kupandishwa vyeo na mzigo mkubwa wa kazi. Otieno alisema KNUT tayari imewasilisha pendekezo la kufupishwa kwa muda wa utekelezaji wa CBA kwa Rais William Ruto na sasa mazungumzo yataendelea kati ya chama hicho, TSC na Wizara ya Elimu. Kwa mujibu wa vyama vya walimu, pamoja na kuboreshwa kwa mishahara, serikali inapaswa kushughulikia pia changamoto nyingine zinazowakabili walimu kama vile uhaba wa wahudumu, huduma duni za matibabu, kuhudumu kwa muda mrefu katika nyadhifa za kaimu bila kunufaika na marupurupu yanayostahili pamoja na mazingira bora ya kazi ili sekta ya elimu iweze kuvutia na kuhifadhi walimu wenye taaluma na uzoefu.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 19 Jul 2026 22:55:07

Kindiki 'akemea' Waziri Ruku kuhusu matamshi yake ya kuleta mgawanyiko Mlimani

MGAWANYIKO wa kisiasa umeibuka ndani ya kambi ya Rais William Ruto baada ya Naibu Rais, Profesa Kithure Kindiki, kupinga hadharani wito wa Waziri wa Utumishi wa Umma, Geoffrey Ruku, wa kutaka Mlima Kenya Mashariki utengane kisiasa na wenzao wa Mlima Kenya Magharibi. Mvutano huo unajiri siku chache baada ya ushindi wa upinzani katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou kufufua mjadala kuhusu mwelekeo wa kisiasa wa eneo la Mlima Kenya, ambalo lina idadi ya juu ya wapigakura. Akizungumza katika ibada ya shukrani ya Dayosisi ya Anglikana ya Embu katika Chuo cha Ualimu cha St Mark's Kigari, Kaunti ya Embu, Profesa Kindiki alisema hataruhusu juhudi zozote za kuligawa eneo hilo kisiasa. "Sitaki watu wetu waanze kuzungumza lugha tofauti. Tumefanya mambo mengi pamoja, tuna historia ndefu na hakuna kinachoweza kuleta mgawanyiko. Kama Naibu Rais nitahakikisha Mlima Kenya unabaki umeungana. Kwa sasa mimi ndiye Naibu Rais na nitahakikisha jamii zetu zinaendelea kutembea pamoja," akasema. Aidha, aliwataka wakazi wa Mlima Kenya kuendelea kumuunga mkono Rais Ruto, akisema hiyo ndiyo njia bora ya kuhakikisha eneo hilo linatoa rais 2032. "Nataka tuwe na mazungumzo ya kweli na watu wetu. Baada ya William Ruto, ni sisi. Ile timu nyingine tuko nambari 20; tutafikiwa baada ya miaka 200," akasema. Kauli ya Profesa Kindiki inaenda kinyume na matamshi ya awali ya Bw Ruku ambaye amekuwa akirindima ngoma ya Mlima Kenya Mashariki kuwa na msimamo wake wa kisiasa na kiuchumi. "Ninapozungumzia mgawanyiko, ninarejelea masuala ya siasa za eneo letu. Nikiona jambo haliko sawa nitalizungumzia." Naibu Rais yuko sahihi kuhusu kuwaunganisha Wakenya," akasema Bw Ruku akikanusha ametofautiana na rais. Baadaye akiwa katika Kanisa la AIC Kabartonjo, Baringo Kaskazini, Bw Ruku alisema Mlima Kenya Mashariki umeamua kubaki ndani ya Kenya Kwanza na hautashawishiwa na kampeni za kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua. Pia alipuuza madai kwamba ushindi wa upinzani katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou unaashiria Rais Ruto amepoteza uungwaji mkono wa Mlima Kenya.  "Gachagua anajigamba baada ya ushindi wa Ol Kalou akidai anadhibiti kura za Mlima Kenya. Kama Raila alikaribia kushinda bila kuungwa mkono na Mlima Kenya, Gachagua anategemea vipi kumshinda Rais Ruto 2027?" akauliza. Kwa mujibu wa mdadisi wa kisisa Prof Gitile Naituli mjadala wa kugawa Mlima Kenya unasukumwa zaidi na maslahi ya kisiasa kuliko maendeleo. "Mtu anayepaswa kuwa na wasiwasi ni Prof Kindiki. Hatakiwi kuruhusu mjadala wa mgawanyiko iwapo ana matumaini ya kumrithi bosi wake mnamo 2032. Hakuna atakayekuchukulia kwa uzito katika siasa za kitaifa ikiwa hujaunganisha ngome yako," akasema

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 19 Jul 2026 21:55:09

Huenda Gachagua akawa debeni 2027 baada ya ushauri uliotolewa na Mwanasheria Mkuu

MAKAHAMA ya Juu imeamuru Mwanasheria Mkuu Dorcas Oduor kutoa ushauri kuhusu mtanziko wa kikatiba unaohusu iwapo maafisa wa serikali waliotimuliwa wanaweza kuwania chaguzi huku wakipinga kufurushwa kwao kortini. Korti Ijumaa iliyopita iliagiza Mwanasheria Mkuu kutoa ushauri katika siku 21. Jopo liliwasilisha suala hilo kwa Mwanasheria Mkuu huku likichelewesha uamuzi muhimu ambao huenda ukaathiri chaguzi kuu zijazo za urais 2027. Kesi hiyo ina umuhimu kwa aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua, aliyekuwa gavana wa Meru, Kawira Mwangaza na aliyekuwa gavana wa Nairobi, Mike Sonko, ambao kung'olewa kwao afisini kumezua makabiliano ya muda mrefu kortini. Kiini cha kesi hiyo ni kuhusu iwapo viongozi waliofurushwa kutoa afisi za umma kupitia mchakato wa sheria wanaweza kuwania afisi za uchaguzi kabla ya kesi zao za rufaa kukamilika. Bw Gachagua alitimuliwa na Bunge la Kitaifa 2024 kabla ya kuwasilisha kesi kortini kupinga uhalali wa kumfurusha. Mvutano huo unaendelea katika Mahakama ya Rufaa. Ni miongoni mwa wapeperushaji bendera wanaodhamiria kupinga kuchaguliwa tena kwa Rais William Ruto, katika uchaguzi mkuu wa Agosti 2027. Bi Mwangaza alitemwa kama gavana wa Meru Agosti 2024 baada ya Seneti kupitisha uamuzi wa bunge la kaunti kumng'atua mamlakani, na kuzua kesi tofauti kortini kuhusu mchakato. Bw Sonko alitimuliwa kama gavana wa Nairobi 2020 na akaendelea kukabiliana kisheria kuhusu ufurushaji wake huku akijihusisha na siasa. Kufuatia kubanduliwa kwao walianzisha vyama tofauti vya kisiasa, huku Bw Gachagua akiwa kinara wa Democracy for the Citizens Party (DCP), Bw Kawira Umoja na Maendeleo Party (UMP) huku Sonko akiongoza National Economic Development Party (NEDP). Kesi iliyo mbele ya Mahakama ya Juu iliwasilishwa na Spika wa Bunge la Kaunti ya Meru, Ayub Bundi Solomon, Aprili 2026 kwa namna ya ushauri wa kurejelewa, akiomba korti hiyo kutafsiri Sura ya Sita ya Katiba pamoja na Vifungu 99 na 193 vinavyosimamia kufuzu na kung'olewa kutoka afisi ya uchaguzi. "Haya ni marejeleo kuhusu ushauri. Marejeleo haya yanatokana na utata ambao haujatatuliwa katika kitovu cha mfumo wa uongozi na uadilifu chini ya Sura ya Sita ya Katiba," anasema. Katika kesi iliyowasilishwa Aprili 10, 2026, Bw Bundi alihoji kuwa amri za korti zinazofutilia mbali ufurushaji zikisubiri rufaa, kimtindo, zimeruhusu maafisa walioondolewa kwa mashtaka ya uadilifu, ikiwemo kutimuliwa, kubaki waliofuzu kwa chaguzi huku kesi zikiendelea. Alifafanua kuwa miaka 15 tangu katiba mpya ilipozinduliwa 2010, "bado hakuna tafsiri thabiti kuhusu ikiwa katiba inabuni kiwango mwafaka kinachoeleweka kuhusu uongozi wa umma hasa kuhusu namna kiwango hicho kinatumika kwa watu waliong'atuliwa afisini." Badala ya kusuluhisha masuala hayo kikatiba papo hapo, jopo la majaji watano wakiongozwa na Naibu Jaji Mkuu Philomena Mwilu waliagiza Spika Bundi kwanza apate ushauri kisheria kutoka kwa Mwanasheria Mkuu kabla ya kesi hiyo kuendelea kusikizwa. "Mlalamishi ameagizwa kutafuta ushauri wa mwanasheria mkuu, na ushauri huo utolewe katika muda wa siku 21 kuanzia tarehe ya uamuzi huu," iliamuru korti. Majaji wengine wa jopo hilo ni Smokin Wanjala, Isaac Lenaola, William Ouko na Mohamed Warsame. Majaji waliagiza kuwa marejeleo na uamuzi uwasilishwe kwa mwanasheria mkuu na kwamba suala hilo lirejeshwe mbele ya Naibu Msajili baada ya kutimiza masharti hayo. Uamuzi huo vilevile uliahirisha kusikiza ombi lililowasilishwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka na Tume ya Maadili ya Kupambana na Ufisadi kujiunga na kesi hiyo. Tume hizo mbili ziliwasilisha ombi kushirikishwa kwa sababu ya majukumu yake kikatiba kuhusu kufuzu kwa mgombea na matakwa ya uadilifu. Spika alihoji kuwa maoni ya Mwanasheria Mkuu kabla ya kuwasilisha marejeleo hayakuwa lazima. Mawakili wake walisisitiza kwamba ushauri tofauti uliotolewa na Korti ya Juu 2024 uliashiria kwamba mchakato si lazima na kwamba muundo wa ugatuzi ulifanya mkondo huo kukosa ustawishaji katika hali hiyo. Majaji walipinga hoja hiyo. "Kanuni 53 ya Sheria za Korti ya Juu 2020, pamoja na orodha ya mamlaka alizonukuu mlalamishi, zinaweka bayana mahitaji ya kutafuta ushauri wa mwanasheria mkuu kabla ya kuwasilisha marejeleo," korti ilisema. Majaji walisema ushauri kama huo, "huenda ukasuluhisha swali lililo mbele yetu kwa namna inayoridhisha mlalamishi, hivyo kuokoa muda muhimu wa korti." Aidha, walihoji kuwa mzozo wa sasa unatofautiana pakubwa na ushauri wa awali kwa sababu mwanasheria mkuu alikuwa mlalamishi katika kesi hiyo na hivyo basi hangetarajiwa kushauri afisi binafsi. Mahakama vilevile ilipuuzilia mbali hoja kuwa mfumo wa ugatuzi unamzuia mwanasheria mkuu kutoa ushauri kuhusu suala hilo. "Mfumo wa ugatuzi jinsi ulivyoundwa kwa sasa haumfungii nje mwanasheria mkuu kutoa ushauri, hasa kwa suala linalohusu umma," majaji walisema. Korti ya juu haikotoa maoni yoyote kuhusu ikiwa maafisa waliong'olewa au kuondolewa mamlakani wanaweza kuwania chaguzi kesi zao za rufaa zikiwa bado hazijakamilika. Badala yake, ilijikita kwenye suala la mchakato lililowasilishwa kwake na kuamuru mwanasheria mkuu kutoa ushauri kwanza kabla ya kikao chochote kuhusu masuala nyeti kikatiba kuendelea. Kesi hiyo imepangiwa kutajwa Agosti

read more